Tafsiri


Historia na maendeleo ya tafsiri ulimwenguni na  nchini Tanzania.

Katika mjadala huu, tutaanza na utangulizi ambapo tutajadili dhana ya tafsiri kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali, pia tutaangalia nini maana ya historia kisha tutaingia katika kiini cha swali kwa kujadili maendeleo ya tafsiri ulimwenguni katika vipindi mbalimbali pia historia na maendeleo ya tafsiri nchini Tanzania na tutaangalia kazi inayoaminika kuwa ndiyo tafsiri na kwanza nchini Tanzania na kisha tutatoa hitimisho la mjadala wetu.

Taaaluma ya tafsiri imeweza kuelezwa na wataalamu mbalimbali kama ifuatavyo:
Mwansoko na wenzake (2006), wanafasili tafsiri kuwa ni zoezi la uhawilishaji wa mawazo katika maandishi kutoka lugha moja hadi nyingine.

AS-Safi akimnukuu Dubois (1974), anaeleza kuwa tafsiri ni uelezaji katika lugha nyingine  au lugha lengwa wa kile kilichoelezwa katika lugha nyingine (lugha chanzi) ikihifadhi maana na mtindo wa matini chanzi.

Catford (1965:20) anaeleza tafsiri ni, Kuchukua mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha moja (lugha chanzi) na kuweka badala yake mawazo yanayolingana katika lugha nyingine (lugha lengwa).
Kutokana na fasili hizo tunaweza kusema kuwa tafsiri ni uhawilishaji wa mawazo, ujumbe, au taarifa iliyopo katika maandishi kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa bila kupoteza maana ya msingi na mtindo uliotumika katika matini chanzi.


Baada ya kujadili dhana ya tafsiri, sasa tunaweza kujadili kwa ufupi kuhusu dhana ya historia.
Wanjala (2011), anaeleza kuwa historia ni taarifa, maelezo na uchambuzi wa matukio, watu na nyakati teule zinazoathiri maisha ya wanajamii husika, sasa na hata siku za usoni.

Historia na maendeleo ya tafsiri ulimwenguni imeelezwa na wataalamu mbalimbali ambao ni kama vile Mwansoko na wenzake (2006), Wanjala (2011), Mshindo (2010), Sofer (2006) ambapo wataalamu hawa wamegawa historia na maendeleo ya tafsiri katika vipindi vifuatavyo:

Enzi za kale. Kipindi hiki kinajumuisha wakati wote wa kihistoria kati ya mwaka 300KK hadi 300BK. Hiki ni kipindi ambacho kilikuwa na maendeleo ya sayansi na taaluma nyingi za kisasa ambapo zinasadikika zilianzia huko Misri. Ugunduzi na ustaarabu ulioletwa na wamisri uliigwa na wayunani na kuwa chimbuko la ustaarabu wa ulaya. Mbinu iliyotumika na wayunani kuchota maarifa ya wamisri ni tafsiri. Wayunani walikaa misri kwa muda na kujifunza lugha ya wamisri na elimu yao. Mambo waliojifunza waliyafasiri kwa kiyunani na kwenda kuyasambaza huko ulaya.

Enzi za giza. Hiki ni kipindi kati ya karne ya 5 hadi 11. Kipindi hiki kiliitwa kipindi cha giza kwasababu kilitawaliwa na misingi ya utamaduni kuoza na uozo wa kijamii kukita mizizi ambapo mambo kama ubashi, ukahaba na unajisi vilikithiri, pia shughuli za elimu zilikwama huko ulaya. Katika kipindi hiki kulikuwa na mapigano kati ya waislamu na wakristo ambapo baada ya mapigano hayo maarifa ya wagiriki yaliyosheheni ujuzi wa sayansi yalifasiriwa kwa kiarabu. Pia baadhi ya mataifa mfano Hispania yalichukua vitabu ambapo vilikuwa vimesheni maarifa ya sayansi na kuyapeleka kwao na kutafsiri katika lugha zao. Tafsiri hizo zilipelekea ulaya kutoka katika kipindi cha giza na kuingia katika kipindi cha ufufuko wa elimu na maarifa. (Renaissance)

Enzi za ufufuko. (Renaissance) inamaana ya ufufuko wa hamu kuu ya elimu na maarifa. Kipindi hiki kilivuma sana ulaya kusini hasa Italia kikiwa na lengo la kufufua shughuli za elimu na utamaduni. Wazungu walipofika Uarabuni walistaajabia elimu ya kisayansi wakayachukua maarifa hayo na kuyafasiri katika lugha mbalimbali mfano kifaransa, kijerumani na kiingereza. Fasili hizo zilizua msisimko wa shughuli za kielimu, maarifa na utamaduni.

Enzi za kati. Hiki ni kipindi kilichoonesha muamko wa kidini katika karne ya 16 ambapo ilianza ujerumani na kusambaa katika maeneo mengine ulimwenguni. Mwamko huu ulipinga muundo, mwelekeo, falsafa na mafunzo mengi ya kanisa katoliki ya wakati huo na matumizi ya lugha moja ya kilatini katika misa na mafunzo. Hali hii ilisababisha mgawanyiko katika dini ya kikristo, watu mbalimbali walitafsiri maandiko matakatifu katika lugha mbalimbali kwa mfano Martin Luther King alitafsiri biblia takatifu kutoka kilatini kwenda kiingereza (1611) ikaitwa The King James Bible, pia alitafsiri biblia kutoka kilatini kwenda lugha ya kijerumani. Baada ya kuona tafsiri ya kilatini imeacha baadhi ya vipengele katika maandiko hayo matakatifu . Jarome alitafsiri biblia ya kigiriki na kiebrania kutoka kwenye lugha ya kilatini

Enzi za kisasa. Kipindi hiki kilikuwepo karne ya 20 ambapo kilijulikana kama kipindi cha tafsiri kutokana na wingi au mfumuko wa tafsiri. Kipindi hiki kimetawaliwa na masafa marefu ya mawasiliano, maendeleo makubwa ya kielimu na ethnolojia, utandawazi na usomi wa lugha, isimu na fasihi. Mikataba ya kimataifa baina ya mashirika ya umma na ya binafsi inafasiriwa kwa yeyote anayehitaji taarifa hizo. Tafsiri ilikolea katika karne hii kutokana na kuzuka kwa mataifa mengi huru yanayoteua lugha rasmi, lugha za taifa na lugha za elimu.

Kwa hiyo baada ya hitaji kubwa la watu kutaka kuwasiliana na jamii au watu wa mataifa, kabila tofauti. Kutokana na hitaji lake kubwa hilo imepelekea taaluma hii kukuwa kwa kasi sana ukilinganisha kipindi cha nyuma  hasa baada ya mapinduzi ya viwanda karne ya 18.
Baada ya kujadili historia na mandeleo ya tafsiri ulimwenguni, sasa tunaweza kujadili historia na maendeleo ya tafsiri nchini Tanzania.

Kwa ujumla historia na maendeleo ya tafsiri nchini Tanzania haina historia ndefu sana kwani inaanzia mnamo karne ya 19 ambapo tunaweza kugawa historia na maendeleo haya katika vipindi vitatu ambavyo, ni kabla ya utawala wa kikoloni, wakati wa utawala wa kikoloni na baada ya uhuru.
Kabla ya utawala wa kikoloni, wamisionari walitafsiri vitabu mbalimbali vya kikristo ikiwemo biblia takatifu kutoka lugha ya kiingereza kwenda Kiswahili na lugha nyingine za makabila kwa lengo la kueneza dini na ustaarabu wa kikristo kwa waafrika.

Wakati wa utawala wa kikoloni, hiki ni kipindi kuanzia miaka ya 1800, katika kipindi hiki wakoloni hasa waingereza walitafsiri maandiko mbalimbali ya kitaaluma na fasihi ya Ulaya kwa lugha ya Kiswahili. Mfano Pia kabla ya uhuru baadhi ya kazi za fasihi zilitafsiriwa kwa mfano tamthiliya ya Mzimu wa Watu wa Kale iliyotafsiriwa na Mohamed S. Abdalla (1960) kutoka lugha ya kiingereza (Shrine of The Ancestors).

Baada ya uhuru ambayo ni kuanzia mwaka 1961, katika kipindi hiki wapo wataalamu waliofanya juhudi za kutafsiri vitabu mbalimbali kwa lugha ya Kiswahili mfano mzuri ni Mwalimu Julius K. Nyerere ambaye alitafsiri vitabu viwili vya mwandishi mashuhuri wa tamthiliya wa huko Uingereza William Shakespeare ambavyo ni tamthiliya ya Juliasi Kaizari (Julius Caesar) (1963) na tamthiliya ya Mabepari wa Venis (The Merchant of Venis) (1969).

Kazi nyingine zilizotafsiriwa baada ya ukoloni ni pamoja na ushairi wa Wimbo wa Lawino iliyotafsiriwa na Paul Sozigwa (1975), kutoka lugha ya kiingereza (Song of Lawino), riwaya ya Uhuru wa Watumwa iliyotafsiriwa na East African Literature Bureau (1967) kutoka lugha ya kiingereza (The Freeing of The Slaves in East Africa). Pia kazi nyingine za fasihi ambazo zimetafasiriwa kwa lugha ya Kiswahili hapa Tanzania ni pamoja na Nitaolewa Nikipenda ambacho kimetafsiriwa na Crement M. Kabugi (1982) kutoka lugha ya kiingereza (I will marry when I Want).

Kwa sasa maendeleo ya taaluma ya tafsiri nchini Tanzania yamepiga hatua kubwa kutokana na kukua kwa sayansi na teknolojia. Taaluma ya tafsiri kwa sasa inafundishwa katika elimu ya sekondari na vyuo mbalimbali. Pia taasisi na asasi zinazojishughulisha na tafsiri zimeongezeka kwa mfano Baraza la Kiswahili la Zanzibar (BAKIZA), Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI), Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA), Taasisi ya Taaluma za Kiswahili (TATAKI) na International Language Orientation Services (ILOS). Pia wapo wafasiri binafsi wanaofasiri lugha mbalimbali kama vile Kiingereza, Kiswahili, Kiarabu, Kifaransa nakadhalika.

Baada ya kujadili kuhusu historia na maendeleo ya tafsiri ulimwenguni na nchini Tanzania, tunaweza kueleza kuwa, kwa hakika ni kazi ngumu kupata kazi ya kwanza kufasiriwa nchini Tanzania, ila kwa kutumia kigezo cha kihistoria tunaweza kusema kwamba kazi ya kwanza kutafsiriwa nchini Tanzania ilikuwa ni biblia takatifu ambayo ilitafsiriwa na wamisionari kutoka katika lugha ya kiingereza kwenda lugha nyingine za makabila kwa lengo la kueneza dini na utamaduni wa kikristo ambayo pia ilikuwa ni njia ya kueneza ukoloni.

Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kuwa taaluma hii ya tafsiri inazidi kukua karne hadi karne kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia yanayofungamana na maendeleo ya taaluma ya lugha na ongezeo la mataifa huru yanayozungumza lugha tofauti. Kwa hiyo tafsiri ni kama nyenzo kuu ya kuunganisha watu wa mataifa haya na hutumika kama njia kuu ya mawasiliano.  

MAREJEO.
As-Safi (1997) “Translation  theories, strategies
Cartford. (1965). A linguistic Theory Translation.
Mshindo. B.H. (2010). Kufasiri na Tafsiri. Oxford University Press. Dar es salaam.
Mwansoko. H.J.M na wenzake. (2006). Kitangulizi cha Tafsiri, Nadharia na Mbinu. TUKI.           Dar es salaam.
Sofer. M. (2006). The Translator’s Handbook. Schreiber Publishing Rockville. U.S.A.
Wanjala, S.F. (2011). Misingi ya Ukalimani na Tafsiri. Kwa shule, vyuo na ndaki. Serengeti                                   Bookshop. Mwanza.


 

 

 

Uainishaji wa matini za tafsiri na mbinu za kutafsiri.

Uainishaji wa matini za tafsiri.

Lengo la mfasiri bora katika kufanya tafsiri ni kutoa zao bora kabisa la tafsiri,  ili kutimiza azma hii hulazimika kuainisha kwanza aina ya matini ya tafsiri kabla hajaanza kufanya tafsiri. Ni muhimu kwa mfasiri yeyote yule kuainisha kwanza aina ya matini kabla hajaanza kutafsiri kwani kila aina fulani ya tafsri huwa na mbinu yake muafaka ya kutafsiri matini husika.
Wataalam wa tafsiri wamejaribu kuainisha matini za tafsiri kwa kutumia mikabala mitatu, mikabala hiyo ni:
(a) Kwa kutumia kigezo cha mada.
(b) Kwa kutumia kigezo cha matumizi ya istilahi.
(c)  Kwa kutumia kigezo cha dhima kuu za lugha.
(a) Kwa kutumia kigezo cha mada.
Kwa kutumia kigezo hiki tunapata aina kuu tatu za matini, mada inayozungumziwa katika matini ndio hutusaidia kujua kuwa hiyo ni aina fulani ya matini, kinachoangaliwa ni maudhui ya matini inayoshughulikiwa. Kwa hiyo kwa kigezo hiki tunapata:
i)          Matini za kifasihi; mfano, riwaya, hadithi fupi, tamthilia n.k
ii)         Matini za kiasasi; mfano, maandiko ya kisiasa na kiserikali kama vile hotuba, risala, propaganda n.k.
iii)        Matini za kisayansi. Matini za namna hii huhusika na fani zote za sayansi kama vile fizikia, kemia, baiolojia n.k.
(b) Kwa kutumia kigezo cha matumizi ya histilahi.
Kigezo hiki huangalia kiwango cha matumizi ya istilahi za uwanja fulani maalum katika matini  husika. Hivyo kutokana na kigezo hiki tunapata makundi matatu; matini zenye kiwango cha juu cha istilahi, matini zenye kiwango cha kati cha istilahi na matini zenye kiwango cha chini cha istilahi. Hivyo kwa kuangalia kiwango cha ujitokezaji wa istilahi katika matini tunapata matini zifutatazo:
i) Matini za kiufundi, hizi zinakuwa na matumizi makubwa ya istilahi.
ii) Matini za nusu ufundi, hizi zinakuwa na kiwango cha kati cha matumizi ya istilahi (zinakuwa na istilahi chache).
iii) Matini zisizo za kiufundi, hizi zinakuwa hazina matumizi ya istilahi na hivyo hutumia msamiati wa kawaida.
(c) Kwa kutumia kigezo cha dhima kuu za lugha.
Kwa mujibu wa Bülher (1965) lugha yoyote ile duniani ina dhima kuu tatu ambazo ni:
i)    Dhima elezi (expresive function). Kazi ya lugha ni kuelezea hisia za mzungumzaji au mwandishi bila kumjali msikilizaji au msomaji. Kiini ni mwandishi au mzungumzaji.
ii)   Dhima arifu (informative function). Hapa lugha hutumika kutolea taarifa. Kiini cha dhima hii ni ukweli wa mambo.
iii)  Dhima amili (provocative function). Lugha hutumika kuchochea hisia za msikilizaji au msomaji. Kiini cha dhima hii ni hadhira.
Kulingana na dhima hizi tatu za lugha tunapata aina tatu za matini ambazo ni:
i)    Matini elezi.
Matini hizi huegemea zaidi upande wa mwandishi, mfano fasihi, maandiko ya kimamlaka kama vile hotuba, mikataba, maandiko ya kisheria, maandiko ya kitaaluma, wasifu, tawasifu, shajara n.k.
ii)   Matini arifu.
Hii ni matini inayokusudia kutoa maarifa kuhusu mada yoyote au jambo fulani. Sifa za matini arifu ni pamoja na kwamba huwa katika muundo maalumu au maumbo sanifu, mfano; kitabu, makala, jarida, ripoti, tasnifu n.k.
iii)  Matini amili.
Matini amili huegemea zaidi upande wa hadhira, mwandishi huchochea hisia za wasomaji ili watende kama yeye anavyotaka. Mfano; mialiko, matangazo, maelekezo (jinsi ya kutumia kitu).
Vigezo hivi vyote vilivyotumika kuainisha matini za tafsiri vyote vinajaribu kuonesha kuwa kuna aina tofautitofauti za matini ambazo mfasri anaweza kukutana nazo. Kwa ujumla matini hizo zinaweza kuwa za kisayansi, za kifasihi au za kisheria.
Kwa misingi hii sisi tunaona kwamba kigezo kizuri zaidi cha kuainisha matini za tafsiri ni kigezo kinachozingatia dhima za lugha, hii ni kwa sababu kigezo hiki kinakwenda mbele zaidi na kuangalia kusudi la matini husika na kwa hiyo hii itamsadia mfasiri kujua nia au kusudi la matini na kumrahisishia kuchagua mbinu inayofaa kufasiri matini husika. Pia vile vile katika kigezo hiki aina zingine za matini zilizoainishwa kwa kuzingatia kigezo cha mada na kigezo cha matumizi ya istilahi huapatikana katika kigezo hiki. Kwa mfano, katika kigezo cha mada tunapata matini kama za kifasihi, kisayansi na kiasasi lakini matini hizi huweza kuainishwa kama matini elezi tunapotumia kigezo cha dhima kuu za lugha.
Kwa hiyo kigezo cha dhima kuu za lugha ni kigezo muafaka zaidi katika uanishaji wa matini za tafsiri kwani hukusanya taarifa nyingi muhimu ambazo huhitajika na mfasiri ili kuteua njia muafaka zaidi katika kufasiri.

Mbinu za kutafsiri.

Baada ya kuangalia aina mbalimbali za matini sasa tuangalie mbinu zinazoweza kutumika katika kufasiri aina fulani ya matini.
Kazi ya kufasiri inahitaji umakini wa hali ya juu; ili kupata tafsiri iliyobora, wataalam wamebuni mbinu mbalimbali za kufasiri kutegemeana na matini husika. Kuna mbinu nne zinazohusika katika tafsiri, mbinu hizo ni kama zifuatazo:
i)    Tafsiri ya neno kwa neno
ii)   Tafsiri sisisi
iii)  Tafsiri ya kisemantiki
iv)  Tafsiri ya kimawasiliano
Hebu sasa tuziangalie kwa kina mbinu hizi na namna zinavyoweza kutumika katika matini ya tafsiri.

i)          Mbinu ya tafsiri ya neno kwa neno.

Hii ni mbinu ambayo kwayo maneno hufasiriwa kwa kuchambuliwa mofimu zinazounda maneno hayo na kwa kuzingatia maana ya msingi/maana ya kikamusi ya maneno katika matini hiyo.
Mfano. 1. Alisafiri kwa basi. Sentesi hii  inaweza kufasiriwa kwa mbinu ya neno kwa neno kama ifuatavyo:
A – li – safiri kwa basi.
S /he |past| travel by bus.
Mfano. 2. Alikunywa maji mengi.
A – li – ku – nyw – a maji mengi.
S /he |past| |inf.| drink water many.
Mfano. 3. Walimpa msukumo mkubwa kwenye biashara yake.
Wa – li – m – p – a msukumo mkubwa kwenye biashara yake.
They |past| |object| |give| pressure big in business his/her.
Mfasiri anayetumia mbinu hii ni lazima achambue mofimu za lugha chanzi na ndipo aandike chini ya matini ya lugha chanzi. Katika mbinu hii muundo wa lugha chanzi utazingatiwa hata kama muundo wa lugha hizo mbili haufanani. Mbinu hii hutumika zaidi katika masuala ya utafiti wa lugha lakini pia huweza kutumika katika hatua za awali mfasiri anapoanza kufasiri matini.
Udhaifu wake.
a)   Mbinu hii haitoi maana kwa uangavu, unaposoma maana haijitokezi.
b)   Maana za misemo na nahau hupotea kwa sababu hutafsiriwa kisisisi.
c)   Husomeka vibaya yaani haina mtiririko unapotaka kufuatilia ujumbe.
d)   Hukiuka muundo wa lugha lengwa na hivyo husababisha kupotea kwa ujumbe uliopkuwa umekusudiwa.

ii)         Mbinu ya tafsiri sisisi.

Hii ni mbinu ambayo hutumika kufasiri maneno yakiwa pwekepweke kwa kuzingatia maana zake za msingi yaani maana za kikamusi. Katika mbinu hii mfasiri anapofasiri huzingatia muundo wa lugha lengwa.
Hebu tuangalie mifano ifuatayo: 
Mtoto wa nyoka ni nyoka.
o   The chilid of a snake is a snake.
Ø  Subira huleta heri.
o   Patience brings blessing.
Ø  Penye nia pana njia.
o   Where there is a will there is a way.
Ø  Mwenda pole hajikwai.
o   He who moves forward slowly does not trip.
Ø  Walimpa msukumo mkubwa kwenye biashara yake.
o   They gave him/her a big push in his/her business.
Mifano hiyo hapo juu huonesha tafsiri sisisi inayvofanyika, licha ya kuzingatia muundo wa lugha lengwa lakini pia mbinu hii ina ubora na udhaifu wake.
Ubora wake ni kwamba maana halisi ya lugha chanzi huzingatiwa kwa kuwa maneno hufasiriwa kwa kuzingatia maana ya msingi.
Udhaifu wa mbinu hii ni kwamba:
a)   Haizingatii muktadha, kwa mfano methali, nahau na misemo pia hufasiriwa kisisi.
b)   Wakati mwingine hutoa tafsiri mbovu, hupotosha ujumbe uliokuwa umekusudiwa.

iii) Mbinu ya tafsiri ya kisemantiki (tafsiri ya wazi)

Katika mbinu hii wafasiri husisitizwa kuzingatia vipengele vyote vya matini chanzi. Kila neno katika matini chanzi hufasiriwa bila kuacha neno lolote. Vipengele vya kisemantiki huzingatiwa kwa ukaribu.

Pia vilevile ni muhimu kuelewa mwandishi alikusudia nini na hivyo kumfanya mfasiri anapofasiri asibadili chochote katika matini chanzi.
Mfano wa tafsiri ya kisemantiki:
Ø  Ilikubaliwa kwamba….
o   It was agreed that….
Ø  Mheshimiwa spika, nachukua nafasi hii…
o   Honorable speaker, I take this opportunity…
Ø  At the end of the day.
o   Mwisho wa siku.
Ø  Ladies and gentlemen.
o   Mabibi na Mabwana.
Faida ya mbinu hii ni kwamba inasaidia kueleza ukweli wa mambo kama ulivyo katika matini chanzi. Pia husaidia kuleta msamiati mwingi katika lugha lengwa, hii ni kwa sababu neno ambalo litakosa kisawe chake katika lugha lengwa litachukuliwa kama lilivyo kutoka katika lugha chanzi na hivyo kuingiza msamiati mpya katika lugha lengwa.
Udhaifu wa mbinu hii ni:
a)   Mbinu hii huweza kusababisha kuwa na matini pana na fafanuzi, matini huweza kuwa ndefu kuliko ile matini ya lugha chanzi.
b)   Huweza kupatikana matini inayosomeka vibaya.
c)   Huwa na mjirudio wa taarifa.
d)   Haihamasishi mfasiri kuzingatia taarifa za kitamaduni.
e)   Maranyingi hutumika kufasiri matini elezi kama vile fasihi, wasifu, tawasifu, nyaraka za kisheria, nyaraka za kisiasa, hotuba n.k.

iv) Mbinu ya tafsiri ya kimawasiliano.

Hii ni mbinu inayotumika katika kufasiri matini ikizingatia zaidi ulewekaji wake katika hadhira lengwa. Mbinu hii husisitiza kuzingatia utamaduni wa lugha lengwa. Zao la tafsiri linatakiwa lieleweke vyema katika lugha lengwa bila ukakasi kwa maana kinachosisitizwa hapa ni uwepo wa mawasiliano yaani ujumbe uliokusudiwa katika lugha chanzi ufike katika lugha lengwa bila kupotoshwa.
Katika mbinu hii mfasiri anakuwa huru kutumia methali, nahau na misemo. Matini zinazofaa katika kutumia mbinu hii ni kama vile matini zenye lengo la kuelimisha au kushawishi au kuarifu.
Mifano ya tafsiri ya kimawasiliano:
Ø  Tanzania National Electric Supply Company Limited.
o   Shirika la umemeTanzania.
Ø  A bird in the hand is worth two in the bush.
o   Fimbo ya mbali haiui nyoka.
Ø  A burnt child dreads fire.
o   Mtoto akililia wembe, mpe.
Ø  Actions speak louder than words.
o   Ada ya mja hunena, mwungwana ni kitendo.
Ø  A drowning man will catch at a straw.
o   Mfa maji haachi kutapatapa.
Ø  All good things come to those who wait.
o   Subira huvuta heri.
Ø  A stitch in time saves nine.
o   Usipoziba ufa utajenga ukuta.
Ø  As you sow, so you shall reap.
o   Mpanda ovyo, hula ovyo.
Ø  Charity begins at home.
o   Kutoa ni moyo si utajiri.
Ø  Clothes don’t make the man.
o   Usichague mchumba siku ya Idi.
Ø  Mtoto wa nyoka ni nyoka.
o   Like father like son.
Ø  Ukistaajabu ya Musa utaona ya Firauni.
o   Wonders never end!
Kwa hiyo mfasiri yeyote yule ni muhimu kuteua mbinu atakayotumia wakati wa kutafsiri kulingana aina ya matini anayotaka kutafsiri. Hata hivyo ni vigumu kutumia mbinu moja pekee katika kutafsiri, kwani mbinu zote huweza kujitokeze katika tafsiri kwa mfano, maneno mengine huweza kufasiriwa kisisi au kisemantiki lakini pia ni lazima iwepo mbini ambayo inatawala mbinu zote. Wataalam wengi wa tafsiri wanapendekeza mbinu ya tafsiri ya kimawasiliano itumike zaidi hususani katika matini zenye lengo la kuelimisha au kuleta athari sawa na ile ile iliyopo katika matini chanzi. Matini kama vile za kisheria mbinu muafaka zaidi ni ile ya kisemantiki.

Zoezi.

1. Taja na fafanua aina za matini ya tafsiri.
2. Kwa kutumia kigezo cha dhima kuu za lugha, taja na fafanua aina za matini za tafsri.
3. Ainisha kigezo kinachofaa kuainisha matini za tafsiri kasha toa sababu kwanini kigezo hicho kinafaa.
4. Taja na fafanua mbinu zinazotumika katika tafsiri.
5. Onesha ubora na udhaifu wa mbinu ya kisemantiki.
6. Tafsiri sentensi ifuatayo kwa kiswahili:
     A habit is a second nature.
       i) Kisisisi……………………………………………………………………
       ii) Kisemantiki……………………………………………………………..
       iii) Kimawasiliano………………………………………………………….
7. Tafsiri sentensi ifuatayo kwa kiingereza:
Maji yakimwagika hayazoleki.
       i) Kisisisi…………………………………………………………………………
      ii) Kimawasiliano…………………………………………

11 comments:

Unknown said...

Asante sana b

Unknown said...

Ungekuwa na kitabu Kaka ingekuwa poa Sana maana nashindwa hate namna ya kuandika reference yako yaa haya matini. Msaada tafadhari

Unknown said...

Hongera sana umejitahidi kuchambua hasa katika kipengele cha mbinu za tafsiri. Mr khalid mwalimu wa kiswahili, glorious academy Zanzibar

Unknown said...

Vizuri sana na hongera umejitahidi sana

Unknown said...

Hongera sana umejitahidi mno,,,,,hadi naona raha kusoma

Mpole Aidan said...

Kazi nzuri. Japo bado napata ugumu kutofautisha tafsiri sisisi na tafsiri ya kisemantiki

Unknown said...

Hongera sana kwa matini yako nzuri juu ya dhana ya tafsiri.

Unknown said...

Hongera3sanaaa umejitahidi kwa kiasi chake

Unknown said...

Asante, umenisaidia. Naomba usikate tamaa endelea.

Unknown said...

Nashukuru sana, nimejifunza mengi,,kweli u mwandishi sugu, hongera

Unknown said...

Shukrani sana kazi yako nimeielewa uasa mbinu za tafsiri