Wednesday, July 17, 2013

MJADALA KUHUSU IDADI YA LAHAJA ZA KISWAHILI NA NAMNA ZILIVYOINUKIA

Dhana ya lahaja
Dhana ya lahaja ni changamani, hutokana na jinsi mtu aliyefasili dhana hiyo anatumia kigezo kipi. Mfano,  kuna kigezo cha isimujamii, hiki ni kigezo cha kuwashirikisha wanajamii au wazungumzaji wa lahaja hiyo na ukapata msimamo wao kuhusu lahaja hiyo. Pia kuna kigezo cha kiisimu; hiki kigezo cha kutofautisha lugha na lahaja nyingine kwa kutumia vigezo vya msamiati wa msingi, fonolojia, pamoja na mofolojia.

Lahaja pia inaweza kufasiliwa kwa kuzingatia utengano wa kijiografia au kijamii. Hii ana maana kwamba unaweza kusikia kuwa lahaja fulani inazungumzwa mahala fulani au huzungumzwa na kundi la watu fulani. Mfano, lahaja ya kitumbatu huzungumzwa sehemu za kisiwa cha Tumbatu vivyo hivyo lahaja ya kipemba huzungumzwa na watu wa Pemba.

Hebu tuangalie uchangamani wa dhana ya lahaja kwa kuangalia fasili zifuatazo:
 Msanjila (2009:124) anasema lahaja ni lugha mojawapo kati ya lugha ambazo kimsingi kuhesabiwa kuwa lugha moja isipokuwa zinatofautiana katika baadhi ya vipengele fulani fulani kama vile lafudhi, fonolojia, msamiati usiokuwa wa msingi au muundo kutokana na eneo lugha hiyo inazungumzwa.

Massamba (2002) anasema kuwa lahaja ni lugha mbalimbali za pwani zilizokuwa na uhusianao wa karibu sana. Lugha hizo ni kama vile ci-mbalazi, ki-amu, ki-mvita, ki-jomvu, ki-mtang’ata, ki-makunduchi, ki-tumbatu, ki-mgao na ki-unguja. Wakati wengine wanaziita lahaja mfano, Polome (1967), Bryan (1959) pamoja na Temu (1980).

Kwa mujibu wa Wikipedia, Kamusi elezo huru  lahaja ni vilugha vidogo vidogo vya lugha moja ambavyo hubainika kijamii au kijiografia.

Ukizitazama fasili hizi kwa makini utagundu kuwa kila mtu ana mtazano wake kuhusu lahaja, wengine wanasema ni vilugha, ni lugha inayojitegemea, wengine wanasema ni tofauti ndogondogo hasa za kimatamshi katika lugha moja. Lakini pia wengine wanaona lahaja ni tofauti za lugha kwa kigezo cha kijiografia na wengine wanaona ni tofauti za kijamii na kijiografia. Kwa hiyo mitazamo hii ndio hulete utata na uchangamani katika kufasili dhana ya lahaja.

Kimsingi fasili iliyotolewa na Msanjila (keshatajwa) inaweza kutusaidia kujua dhana ya lahaja kwani fasili hii ni ya kiutendaji.Kwa hiyo lahaja ni lugha mojawapo kati ya lugha ambazo kimsingi kuhesabiwa kuwa lugha moja isipokuwa zinatofautiana katika baadhi ya vipengele fulani fulani kama vile lafudhi, fonolojia, msamiati usiokuwa wa msingi au muundo kutokana na eneo lugha hiyo inamozungumzwa.

Mjadala kuhusu idadi ya lahaja za kiswahili na namna lahaja hizi vilivyoinukia:
Mjadala hu ulianza siku nyingi kidogo na hadi sasa hivi hakuna utafiti wa hivi karibuni unaoweza kutusaidia kuthibitisha idadi kamili za lahaji za Kiswahili. Hebu tuangalie wataalam jinsi wanavyojadili idadi ya lahaja za Kiswahili.

Chiraghdin na Mnyampala (1977) wametaja idadi ya lahaja ishirini, lahaja hizo ni kama vile; Kiunguja, Kimrima, Kimgao, Kimvita, Kihadimu, Kipemba, Kirumba, Kiamu, Kipate, Kisiu, Kitikuu, Kingazija, Kingozi, Kitumbatu, Kimtang’ata, Chichifundi, Chibalanzi, Kingwana, Kinyare, na Kijomvu.

Nurse na Spear (1985) wametaja idadi ya lahaja kumi na sita (16), na wamezigawa katika makundi mawili ambayo ni kundi la kaskazini na kundi la kusini. Mfano kundi la kaskazini lina lahaja saba (7) wakati kundi la kusini lina lahaja tisa (9). Baadhi ya lahaja hizo ni;- Kipate, Chimiini, Kibajuni, Kisiu, Kijomvu, Chifunzi, Kipate, Kiunguja, Kimtang’ata, Kimakunduchi na kuendelea.
Utata kuhusu idadi za lahaja za kiswahili unatokana na sababu zifuatazo;

Kigezo kilichotumika katika kufanya utafiti wa lahaja za kiswahili. Unaweza kufanya utafiti wa lahaja za kiswahili kwa kutumia kigezo cha kijiografia, kijamii, pamoja na kiisimu. Vigezo hivyo vyote vinaweza kukupatia idadi tofauti za lahaja mfano, Massamba katika utafiti wake kwa kutumia kigezo cha kiisimu (1977) alifanya utafiti katika jamii za chi-ruri, chi-jita, na ki-kwaya akathibitisha kuwa hizi ni lahaja za lugha moja na si tofauti, pia kwa kutumia kigezo cha utengano wa kijiografia na kijamii mfano katika lugha ya Kiswahili kwa kiasi kikubwa uanishaji umefanywa kwa utengano wa kijiografia kama vile,  kipate kinazungumzwa sehemu za Pate na lahaja ya kipemba huzungumzwa  Pemba. Hivyo kutokana na sababu kama hizi husababisha watafiti wengi kutofautiana katika kupata idadi kamili za lahaja.