Sunday, December 9, 2012

TAFSIRI KATIKA KISWAHILI



Tafsiri ni taaluma ya lugha ambayo imefuata taaluma ya ukalimani, ni taaluma iliyoanza baada ya ugunduzi wa maandishi. Tafsiri za mwanzo kabisa ni zile zilizohusu maandiko ya kiyahudi, kwa mfano tafsiri ya kwanza kufanyika katika nchi za magharibi ni ile ya tafsri ya maandiko ya kiyahudi yaliyotafsiriwa katika lugha ya kigiriki cha koine kati ya karne ya 3 na ya 1 kabla ya kristo.

Maana ya tafsiri.

Kwa mujibu wa mtandao wa Wikipedia, tafsiri ni mawasiliano ya maana iliyokatika matini ya lugha chanzi kwa njia ya kuweka maana inayolingana katika matini ya lugha lengwa.
Naye Mwansoko (2006) anasema tafsiri ni zoezi la uhawilishaji wa mawazo katika maandishi kutoka lugha moja hadi nyingine.
Kihore (1989) anafasili tafsiri kama jaribio la kuhawilisha ujumbe katika maandishi kutoka lugha moja kwenda nyingine.
Kwa ujumla fasili hizi zote ni nzuri kwani zote zimeonesha kuwa tafsiri hufanyika katika maandishi. Kwa hiyo tunaweza kusema kuwa tafsiri ni zoezi la uhawilishaji wa maana, mawazo, dhana au ujumbe ulio katika maandishi kutoka lugha chanzi na kuweka badala yake maana, ujumbe, mawazo au dhana inayolingana na ile ya lugha chanzi katika lugha lengwa.

Dhima ya tafsiri.

Tafsiri kama taaluma ya lugha ina majukumu kadhaa ya kuyashughulikia, majukumu hayo ni kama yafuatayo:
·         Tafsiri ni njia ya mawasiliano baina ya watu wanaozungumza luga tofauti.
·         Tafsiri inatumika kutolea matangazo, mfano, utalii, brosha na kadhalika.
·         Ni kama nyenzo ya kukuza fasihi. Mfano, hadithi ya alfu lela ulela ( siku  elfu moja), treasure island (kisiwa chenye hazina), Robinson Krusoe na kisiwa chake, mabepari wa venisi n.k. waandishi waliweza kuiga mbinu za uandishi na hivyo kuwa na fasihi bora.
·         Ni nyenzo ya kueneza utamaduni, mfano dini za kigeni kama vile ukristo na uislam uliingizwa kwa njia ya tafsiri na ukalimani.
·         Ni nyenzo muhimu ya kujifunza lugha ya kigeni na kujifunza miundo na maumbo ya lugha fulani. Mfano watu wanaofanya utafiti kuhusu luhga fulani hutumia tafsiri kama njia ya kuelezea lugha hizo.
·         Tafsiri humwezesha mtu kujiajiri (kama chanzo cha ajira). Mfasiri anapofanya kazi ya kufasiri anapata pesa na hivyo hizo pesa humsaidia katika maisha yake ya kila siku.
·         Ni kama njia ya kukuza lugha; msamiati mwingi huingia katika lugha lengwa na hivyo kuitajirisha.

Sifa za mfasiri.

Ili mtu kuitwa mfasiri anatikwa awe na sifa zifuatazo:
·         Awe anamudu vizuri sarufi za lugha zote mbili anazofanyia kazi.
·         Awe ana ufahamu wa kutosha juu ya utamaduni wa lugha chanzi.
·         Awe ni mtumiaji mzuri wa kamusi na marejeo mengine muhimu.       
·         Awe na uwezo mkubwa wa kuandika katika lugha chanzi.
·         Angalau awe na ujuzi wa kutumia kompyuta.


Mambao ya kuzingatia wakati wa kutafsiri.

Kuna mambo muhimu ambayo mfasiri anatakiwa kuyazingatia katika kufasiri matini, mambo hayo ni kama yafuatayo:
a)   Mfasiri atalazimika kusoma matini yote kabla hajaanza kufasiri. Atalazimika kufanya hivyo ili kufanya yafuatayo:
·         Ili aweze kuelewa kinachozungumzwa – ujumbe uliomo.
·         Aweze kuandaa marejeo muhimu anayohitaji k.v. kamusi, vitabu n.k.
·         Ili aweze kubaini aina ya matini.
·         Ili aweze kubaini matatizo yanayojitokeza katika matini husika na kuweza kuyatatua matatizo hayo, mfano; matatizo ya kitahajia tungo ambazo hazijakamilika n.k.
·         Ili kusaidia kuigawa kazi; kama ni kazi ndefu anaigawa katika vipande fulanifulani hasa kama kazi ni ya watu wengi.

Friday, March 16, 2012

KISWAHILI NA UKALIMANI

Dunia inabadilika kila kukicha, sayansi na teknolojia huibuliwa kila kukicha, mambo haya yote huwaweka watu pamoja kutoka kila kona ya dunia, lakini pia watu hawa hawzungumzi lugha moja, wanahitaji kuwasiliana na ili mawasiliano yaweze kufanyika lazima kuwepo na lugha inayowaunganisha. Suala hili ni gumu kwa kuna lugha nyingi sana duniani na kila nchi inasera yake juu ya lugha lakini pia lazma watu wawasiliane na hapa ndipo tunaona umuhimu wa kuwepo mkalimani. 
Lugha ya kiswahili inakuwa kwa kasi sana, vyuo mbalimbali duniani hufundisha lugha hii adhimu kwa nini wewe usione fursa hii na uchukue hatua ya kujifunza ukalimmani ili ujiajiri katika soko kubwa kama hikli.
Kabla hujachukua uamuzi hebu jielimishe kidogo juu ya taaluma hii ya ukalimani.


Tafsri na ukalimani ni taaluma za lugha ambazo mara nyingi watu huchanganya wakidhani kuwa dhana hizi mbili hufanana lakini kimsingi kuna utofauti mkubwa kati ya tafsiri na ukalimani, elimu na ujuzi katka taaluma hizi hutofautiana. Kuna tofauti za msingi zinazotofautisha taaluma hizi, tutazichambua kwa kina katika sura zinazofuata. Kwa sasa tuangalie kwa kina dhana nzima ya ukalimani ambapo tutaangalia maana, aina za ukalimani, sifa za mkalimani (mambo ya kuzingatia katika ukalimani) na mwisho hitimisho.
Maana ya ukalimani.
Ukalimani wa lugha hulenga kurahisisha mawasiliano ya lugha ya mdomo au lugha ya alama kati ya watumiaji wa lugha mbili tofauti.
Kwa mujibu wa Encarta (2009) ukalimani ni tafsiri ya mdomo ya kile kinachosemwa katika lugha moja kwenda lugha nyingine ili kusudi wazungumzaji wa lugha tofauti waweze kuwasiliana.
Wikipedia wamefasili ukalimani kuwa ni uhawilishaji wa ujumbe katika lugha ya mazungumzo au lugha ya alama kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine.
Fasili zote hizi zinajaribu kutupa mwangaza hasa juu ya maana ya ukalimani, fasili ya kwanza inakasoro. Kutumia istilahi yenye maana tofauti na kile kinachojaribu kufasiliwa huleta mkanganyiko, istilahi tafsiri inamaana tofauti na ukalimani kwa hiyo sio sahihi kuitumia katika kufasili dhana ya ukalimani. Fasili ya pilli imejaribu kugusa mambo muhimu katika dhana ya ukalimani, kwamba ni uhawilishaji wa ujumbe katika lugha ya mazungumzo, kimsingi ukalimani hufanyika katika lugha ya mazungumzo.
Kwa hiyo kutokana na fasili hizi tunaweza kupata fasili ya jumla kwamba, ukalimani ni zoezi la uhawilishaji wa mawazo,ujumbe, maana katika lugha ya mazungumzo au lugha ya alama kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa.
Hivyo basi mkalimani ni mtu ambaye huhawilisha mawazo, maana au maelezo kutoka lugha chanzi na kuyaweka mawazo au maelezo au maana yenye maana inayolingana katika lugha lengwa, katika wakati halisi. Kazi ya mkalimani ni kufikisha kila kipengele cha kisemantiki (rejesta,toni) na kila lengo na hisia za ujumbe ambao mzungumzaji wa lugha chanzi amekusudia kufikisha katika wapokeaji wa lugha lengwa.
Aina za ukalimani.
Kuna aina tofautitofauti za ukalimani kulingana na vigezo tofautitofati vinavyotumika katika kuainisha aina za ukalimani. Kwa kutumia kigezo cha jinsi ukalimani unavyofanywa, tunapata aina kuu mbili:
Ukalimani mfululizo; katika ukalimani wa aina hii mzungumzaji wa lugha chanzi na mzungumzaji wa lugha lengwa huanza pamoja na kumaliza pamoja. Maranyingi vifaa maalum hutumika, mkalimani hukaa katika chumba chenye kidhibiti sauti akizungumza kupitia kipaza sauti wakati huo akimsikia na kumwona barabara mzungumzaji wa lugha chanzi kupitia visikizio. Wasikilizaji wa lugha lengwa hupata ujumbe kupitia visikizio. Vilevile ukalimani wa aina hii hutumiwa sana na wakalimani wa lugha ya alama.
Ukalimani fuatizi; katika aina hii ya ukalimani, mkalimani huzungumza baada ya mzungumzaji wa lugha chanzi kumaliza kuzungumza. Mkalimani anakua amesimama au amekaa sambamba na mzungumzaji wa lugha chanzi akiwa anasikiliza napengine kuandika maneno anayozungumza mzunguzaji wa lugha chanzi ili kumsaidia kukumbua pindi atakapoanza kukalimani. Wakati mzingumzaji wa lugha chanzi anapumzika au anamaliza kuongea ndiposa mkalimani anahawilisha kipande cha ujumbe au ujumbe mzima katika lugha lengwa.

Aina zingine za ukalimani.
Ukalimani wa kwenye mikutano; huu ni ukalimani unaofanyika wakati wa mikutano, huweza ukawa fuatizi au mfululizo, lakini kwa sababu ya mikutano inayokutanisha lugha nyingi, ukalimani fuatizi hautumiki. Katika ukalimani wa kwenye mikutano maranyingi mkalimani hufanya ukalimani kutoka lugha za kigeni kwenda lugha yake ya asili.
Ukalimani wa mahakamani; ukalimani wa aina hii hufanyika mahakamani, katika mabaraza ya kutolea hukumu na mahali popote pale ambapo masuala ya kisheria hufanyika, mfano katika kituo cha polisi hususani wakati wa kuchukua maelezo au katika ukumbi wa mikutano kwa ajili ya kuapishwa.
Ukalimani kiungo; ukalimani wa aina hii ni pale ambapo mkalimani humsaidia mtu au kikundi cha watu katika kutalii, matembezi au katika mkutano.
Ukalimani wa lugha ya alama; hii ni aina ya ukalimani ambao hufanyika kati ya lugha ya alama na lugha ya mazungumzo. Mzungumzaji anaweza kuongea mkalimani akahawilisha mawazo kwa njia ya alama, vilevile wakati mtu asiyesikia akifanya mawasiliano kwa lugha ya alama, mkalimani atahawilisha maana katika lugha ya mazungumzo. Vilevile ukalimani huweza kufanyika kati ya lugha ya alama na alama hii ni kwa sababu lugha ya alama hutofautiana kati ya nchi na nchi.
Ukalimani wa vyombo vya habari; kulingana na asili yake ukalimani wa vyombo vya habari hufanyika kwa ukalimani mfululizo. Hufanyika zaidi katika matangazo ya moja kwa moja ya televisheni au redio. Katika ukalimani wa vyombo vya habari vifaa kama  chumba cha kudhibiti sauti, kiwamba nakadhalika huhitajika sana.
Ukalimani wa simu; ukalimani wa aina hii humsaidia mkalimani kufanya ukalimani kupitia simu. Maranyingi hufanyika katika mazingira ambayo watu wanaohitaji kuwasiliana tayari wanakuwa wamekwishazungumza kupitia simu.
Ukalimani wa video; ukalimania wa aina hii hufanyika katika mazingira ambapo mmoja kati ya wanaowasiliana ni kiziwi au hasikii vizuri au hawezi kuongea (bubu). Katika mazingira kama haya ukalimani wa lugha ya alama hufanyika zaidi.
Ukalimani kulingana na muktadha; katika kundi hili kuna aina nyingi kulingana na jinsi itakavyojidhihirisha aktika miktadha tofautitofauti. Mfano, ukalimani wa kanisani, ukalimani wa msikitini, ukalimani wa mahakamani, jeshini nakadhalilka.
Ni matumaini ya ngu utakuwa umenufaika, unaweza pia kutoa maoni yako!.