Kiswahili na TEHAMA



MAENDELEO YA KISWAHILI KATIKA TEKNOLOJIA YA HABARI NA MAWASILIANO (TEHAMA)
Aritamba Malagira
Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam
           
             Ikisiri
Teknolojia ya habari na mawasiliano imekuwa ikikua kila siku kutoka simu ya kukoroga hadi simu ya mkononi, matumizi ya wavuti na nyinginezo nyingi, kwa kweli ni hatua kubwa ya maendeleo katika teknolojia. Hivi sasa watu wanawasiliana ndani ya sekunde chache kwa umbali wa kutoka bara hadi bara kupitia wavuti. Katika hali kama hii lugha za ulimwengu nazo zimekuwa zikijitahidi kukabiliana na ukuaji huu wa teknolojia kwa kutafuta istilahi mpya ili kuelezea dhana mpya za kiteknolojia zinazoibuka. Katika harakati hizi, Kiswahili hakiko nyuma, istilahi mpya za Kiswahili zimekuwa zikiundwa ili kukidhi haja ya kuwasiliana kupitia Teknolojia ya habari na mawasiliano. Makala hii inalenga kuangalia hatua iliyofikiwa na Kiswahili katika tasnia ya teknolojia ya habari na mawasiliano ikiwa ni pamoja na kuchunguza istilahi za ki-TEHAMA zinazotumika.

1.      Utangulizi
Teknolojia ya habari na mawasiliano imekuwa kiungo muhimu sana katika maendeleo ya watu duniani. Watu wamekuwa wakitumia teknolojia hii katika kufanya mawasiliano muhimu, kufanya bishara na mambo mengine mengi yanayowanufaisha watu. Kompyuta/ Talakirishi ni moja ya kifaa kilicholeta mapinduzi katika TEHAMA kama asemavyo Katambi (2011) “Kompyuta ama Tarakilishi katika lugha ya Kiswahili ni kifaa ambacho kimebadilisha kabisa mfumo wa maisha ya binadamu katika miongo takribani sita iliyopita. Kutokana na kuwapo kifaa hiki dunia imejikuta katika maendeleo makubwa kabisa kuliko kipindi chochote kile katika historia ya kuwapo kwake. Kifaa hiki kimeleta mabadiliko makubwa Sana katika maisha ya kawaida ya binadamu. Kifaa hiki kimesababisha mambo mengi kufanyika katika hali ambayo hakika isingewezekana au ambayo awali ingeonekana kama ya kufikirika!. Kompyuta imeyafanya maisha kuwa rahisi zaidi. Kompyuta imeifanya dunia kuwa Kama kijiji kidogo ambacho unaweza kukizunguka katika muda mfupi Sana wa sekunde chache”. Maneno haya ya Katambi yanaonesha ni jinsi gani kompyuta ilivyo muhimi katika TEHAMA, mawasiliano yote ya teknolojia ya habari hufanywa kwa kutumia kompyuta, mfano; matangazo ya redio na televisheni, magazeti  na n.k huandaliwa kwa kutumia kompyuta na kuwa tayari kwa ajili ya kupasha habari.
Makala hii, kwa kuzingatia umuhimu wa TEHAMA katika dunia ya sasa imejikita katika kuchunguza maendeleo ya Kiswahili katika uga wa habari na mawasiliano kwa umahususi zaidi katika mawasiliano yanayohusisha matumizi ya kompyuta hususani wavuti na programu nyingine za kompyuta. Tutaangalia umuhimu wa matumizi ya Kiswahili katika TEHAMA, maendeleo yaliyofikiwa, changamoto na mwisho ni hitimisho.
  
2.      Usuli
Neno Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ujumla wake hurejelea mifumo yote ya kiteknolojia inayotumika kutengeneza, kuhifahdi, kuchakata na kutumia habari katika mifumo yake tofautitofauti (data, picha, uwasilishaji wa medianuwai na mifumo mingine mingi) na mabayo huwezesha, kurahisha na kutegemeza mawasiliano. Kwa umahususi zaidi, TEHAMA inarejelea kukutana au kuingiliana kwa mikroelektroniki,  talakirishi  na mawasiliano ya kutumia redio, simu au televisheni ambavyo hufanya kuwezekana kwa data, ikiwa ni pamoja na matini, video na ishara za video kuweza kusafirishwa mahali popote duniani ambapo ishara za kidijitali huweza kupokelewa… (Howell na Lundall, wakinukuliwa na Akinyi 2010). Kwa ujumla TEHAMA inahusu mambo mengi sana, matumizi ya kompyuta, wavuti, matangazo ya redio na televisheni, satelaiti, picha na mambo mengine mengi yafananayo na hayo hujumuishwa katika teknolojia ya habari na mawasiliano.
2.1  Umuhimu wa TEHAMA katika maendeleo kwa ujumla
Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa ujumla imechangia sehemu kubwa kuleta maendeleo hasa katika kipindi hiki cha karne ya 21 ambapo utandawazi umeenea ulimwengu mzima na kuifanya dunia kuwa kama kijiji ambapo watu huwasiliana na kufanya kazi na biashara kwa pamoja kama wapo katika kijiji kimoja, mambo haya yote yanafanikiwa kwa kuwezeshwa na TEHAMA. Kama asemavyo Kamau (2009) kuwa ushirikiano wa kimataifa katika mambo kama vile siasa, biashara, uchumi , michezo n.k  huwezeshwa na kurahisishwa na teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) ambayo imeuunganisha ulimwengu mzima kimawasiliano. Kwa maelezo  haya tunaweza kuona ni jinsi gani TEHAMA ilivyo kuwa muhimu katika ulimwengu wa sasa.
Lugha ni muhimu sana katika suala zima la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano hatuwezi kuhamisha maarifa yaliyopo katika teknolojia hii bila kutumia lugha na kwa hiyo ili kuwapo na maendeleo endelevu kupitia TEHAMA ni lazima pia lugha inayotumika kuhamisha maarifa ya teknolojia hii iwe inaleweka kwa watumiaji husika. Hii itakuwa rahisi kwao kuilewa na kuitumia teknolojia hii vilivyo kwa sababu lugha inayotumika ni lugha wanayoifahamu na ni lugha yao.
Kama tujuavyo bara la Afrika halijaendelea sana kwa kiwango cha kuzalisha teknolojia zitakazo kubalika katika masoko ya kimataifa kama yafanyavyo mabara mengine hususani mabara ya Ulaya na Marekani, kwa hiyo kulingana na hali hii Afrika imekuwa ikiingiza teknolojia za kigeni kutoka Mabara mengine hasa Marekani na Ulaya, teknolojia hizi zimekuwa zikiingizwa kwa lugha za kigeni jambo ambalo hufanya watumiaji wengi wa Waafrika kushindwa kumudu matumizi ya teknolojia hizi kwa sababu hawajui lugha iliyotumiwa. Kwa mfano kompyuta zinazoingizwa Afrika programu zake huwa zimeandikwa kwa lugha za kigeni hususani kiingereza, watu mabao wataweza kuzitumia kwa urahisi ni wale ambao wanazijua lugha hizi vilivyo na kuwaacha wale wasiojua wakiwa wameduwaa ambao kimsingi ni wengi kuliko wale wanaojua. Kwa hiyo, ili kuondokana na tatizo hili, upo umuhimu mkubwa wa kuziendeleza lugha za Kiafrika kiteknolojia. Suala hili ni la msingi sana, kwani kwa kufanya hivi hatutakuwa tumeendeleza lugha tu bali pia tutakuwa tumeindeleza jamii yetu kiteknolojia.
2.2 Kwa nini Kiswahili katika TEHAMA
Wataalam wengi wanipigia upatu lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya utandawazi barani Afrika, hii ni kwa sababu lugha ya Kiswahili imeendelea sana kuliko lugha nyingine za Kiafrika na ndiyo lugha pekee iliyoonekana kuwa tayari kupokea kwa haraka mabadiliko ya kiteknolojia yanayoibuka kila siku duniani. Kwa maana kwamba lugha ya Kiswahili ina utajiri mwingi wa msamiati kiasi cha kukabiliana na teknolojia za kigeni zinazoibuka bila matatizo yoyote. Kama asemavyo Kamau (2009) “kwa vile utandawazi huhusika na uunganishaji wa mataifa mbalimbali, basi Afrika yahitaji lugha moja yenye asili ya Kiafrika kama lugha ya kusambaza utandawazi. Kwa sasa mfano mzuri wa lugha kama hii ni lugha ya Kiswahili. Lugha hii ndio lugha kutoka barani Afrika ambayo ina matumizi mapana kuliko lugha nyingine hapa barani na kwingineko”. Nukuu hii inatuonesha ni jinsi gani lugha ya Kiswahili ilivyo muafaka katika suala zima la utandawazi wa Afrika. Kimsingi utandawazi husambazwa kupitia lugha na teknolojia, kwa hiyo tunaweza kuona jinsi lugha ilivyo chombo muhimu sana katika maendeleo ya teknolojia na kwahiyo Kiswahili kama lugha ya kiafrika ni muhimu iwe imejiendeleza na kujitosheleza kiteknolojia kwaajili ya mahitaji ya watu wake.
Kutokana na umuhimu wa TEHAMA kama ilivyofafanuliwa hapo juu na kutokana na  umuhimu wa lugha katika maendeleo ya kiteknolojia, tunaweza kuona jukumu la lugha ya Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Lugha ya Kiswahili imebeba jukumu kubwa la kuhakikisha wakazi wa Afrika Mashariki wanaipata na kuitumia teknolojia mpya kwa lugha wanayoifahamu ambayo ni Kiswahili. Kwa kufanya hivi matumizi ya teknolojia yataimarika katika ukanda huu wa Afrika Mashariki. Kwa misingi hii naweza kusema ndio sababu pekee iliyonisukuma kuichunguza lugha ya Kiswahili katika uwanja wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

3.      Hatua iliyofikiwa na lugha ya Kiswahili katika TEHAMA
Kwa kweli lugha ya Kiswahili imepiga hatuta kubwa sana katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Kama tulivyo kwisha kusema huko awali kwamba TEHAMA ina uwanja mpana sana, tunapozungumzia TEHAMA tunazungumzia vitu vingi sana kama vile matangazo ya redio na televisheni kwa namna yanavyofanywa, matumizi ya kopmyuta kwa namna yake n.k. Katika makala hii tutajikita zaidi katika matumizi ya kompyuta kwa namna yake, tutajikita hapa kwani hii ndio inaonekana kuwa teknolojia mpya kabisa katika mazingira ya lugha ya Kiswahili na dhana mpya zinazidi kuibuliwa kila siku katika matumizi ya kompyuta.
Kompyuta kimekuwa kifaa muhimu sana katika shughuli nyingi za kimaendeleo, kwa kutumia kompyuta watu wamekuwa wakifanya mambo chungu nzima na kwa urahisi sana. Bila shaka umekwisha sikia kuwa unaweza kununua bidhaa kwa kutumia kompyuta ukiwa nyumbani kwako bila ya hata kwenda huko sokoni au dukani. Bila shaka umekwisha sikia kuwa mabenki, hospitali, taa za kuongozea magari barabarani, kamera za usalama, ndege za abiria na kivita na hata lift unazopanda kila siku unapoingia na kutoka ofisini katika jengo refu huendeshwa kwa msaada wa kompyuta. Bila shaka umekwisha jionea mwenyewe au kusikia habari kama hizi. Umekwisha sikia kuwa mtu anaweza kumchagua mgombea wa urais au ubunge kwa kutumia kompyuta! Haya na mambo chungu nzima hufanyika kwa msaada wa kompyuta. Katika nchi zilizoendelea matumizi ya kifaa hiki yanaendelea kushika hatamu kiasi kwamba kila kitu sasa kinafanywa Kwa kutumia mashine zinazoongozwa kwa kompyuta.
Kwa hiyo unaweza kuona ni jinsi gani matumizi ya kompyuta yalivyokuwa muhimu sana katika maisha ya kila siku. Serikali za Jumuia ya Afika mashariki zimekuwa zikisisitiza matumizi ya kompyuta kuanzia shule za awali, kwa kuzingatia kwamba matumizi ya kompyuta yameongezeka sana katika ulimwengu wa sasa lakini changamoto zinazoikabili progaramu hii imekuwa ni lugha ya kufundishia. Kwa mfano Tanzania somo la TEHAMA linafundishwa kuanzia shule za msingi; shule za msingi kwa Tanzania hutumia lugha ya Kiswahili kama lugha ya kufundishia na   kwa kuwa programu za kompyuta zimeandikwa kwa kiingereza, italazimika programu hizo zitafsriwe katika Kiswahili ili ufundishaji uweze kuwa rahisi. Na hapa ndipo tunapata istilahi mpya za Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
Licha ya uhitaji wa kufundishwa somo la Kiswahili katika shule za awali lakini pia makampuni makubwa yanayohusika na mawasiliano ya kompyuta yamekuwa yakitafuta nija ya kujiimarisha kibishara katika maeneo mbalilimbali duniani. Mbinu moja wapo amabyo wemekuwa wakiitumia ni kuhakikisha wateja wao wanapata huduma kwa lugha yao. Kwa mfano kampuni ya Microsoft kwa mara ya kwanza kabisa katika historia ilianzisha mradi wa kutafsiri program zake kwa Kiswahili. Kama asemavyo King’ei (2010) “kampuni ya talakirishi iitwayo microsoft ilitekeleza hatua ya kihistoria  mwaka 2005 kwa kuanzisha kamusi maalumu inayowawezesha watumiaji wa talakirishi kutumia lugha ya Kiswahili katika mawasiliano yao yote kwa kompyuta. Programu hii mpya inamwezesha mtumiaji kompyuta asiyefahamu lugha nyingine kama vile kiingereza kutumia kompyuta na kuwasiliana bila shida yoyote”.
Msanjila na wenzake (2011) pia wanasema hadi wakati huu lugha ya Kiswahili imekwisha ingizwa katika mifumo miwili ya kompyuta ijulikanayo kama linuksi na mikrosofti. Wanaendelea kusema, kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo hii maana yake ni kwamba mtumiaji anaweza kuvinjari mifumo hiyo ya kompyuta kwa Kiswahili akiamua kufanya hivyo.
Kwa mujibu wa maelezo ya wataalamu hawa ni wazi kwamba mpaka sasa hivi Kiswahili kinatumika katika baadhi ya mifumo ya kompyuta. Katika kufanikisha hili ujanibishaji wa programu kadhaa za kompyuta ulifanyika. Kahigi (2007) anasema “Mradi wa ujanibishaji wa Office 2003 na Windows XP kwa Kiswahili sanifu ulitekelezwa katika kipindi 2004-2005. Malengo ya maradi yalikuwa: (1) kuandaa istilahi za kompyuta kwa Kiingereza-Kiswahili, na (2) kutafsiri programu nne za kawaida za Office (Outlook, Excel, Word na PowerPoint) na Windows XP”. Hii inamaanisha kwamba programu hizi zinapatikana katika lugha ya Kiswahili. Hebu tuangalie mifano ya istilahi kutoka katika programu hizi za Office 2003 na Windows XP kama zilivyoorodheshwa na Kahigi, ni istilahi zaidi ya 600 lakini hapa tutaangalia chache tu:
  1.   Fikia                          Access 
  2.   Kibonye fikishi        Access key 
  3. Viziada                    Accessories 
  4.  Amilisha                  Activate 
  5. Kirekebu                 Adapter 
  6. Kihadharishi           Alert box 
  7. Program matumizi  Application 
  8.  Makaaba                   Archive 
  9. Vitome mchoro       Bit map 
  10. Kiashiri mada        Book mark 
  11. Sakura                    Browse 
  12. Kisakuzi                  Browser 
  13.  Kwa kaida              By default 
  14.   Msabidi                  Configuration 
  15. Sabidi                     Configure 
  16. Puna                       Crop 
  17. Kielekezi                Cursor 
  18. Tanafsi                   Custom 
  19. Pakua                     Download 
  20. Kijachini                Footer 
  21. Nakala bayana     Hard copy 
  22. Kidakuzi                 Cookie 
  23. Sanidi                     Install 
  24. Kicharazio             Keyboard 
  25. Kiolezo                  Template 
  26. Tafutatua               Trouble-shoot 
  27. Sanidua                  uninstall 
  28. Sasaisha                  Update 
  29.  Kidhulishi                Highlighter 
  30. Kichapishi                Printer 
  31. Kingavirusi              Antivirus     
Hizi ni baadhi tu ya istilahi kati ya nyingine nyingi zilizoundwa katika mradi wa kujanibisha programu za office 2003 na Windows XP. Jitihada za kampuni ya Microsoft hazikuishia hapo tu, mnao mwezi mei mwaka 2011 kampuni hii ilizindua programu ya Windows 7 kwa Kiswahili, hatua hii imezidi kukiimarisha Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Haya ni maendeleo makubwa katika lugha ya Kiswahili. Kwa hiyo sasa mtumiaji wa Kiswahili anachaguo la kufanya, ama kuendelea kutumia programu hizi kwa lugha ya Kiingereza au kwa lugha ya Kiswahili.
4.      Changamoto zinazoikabili lugha ya Kiswahili katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
Kila jitihada zinazofanywa katika kufikia malengo fulani huwa hakukosi changamoto. Katika jitihada za kufanya Kiswahili kuwa lugha ya kiteknolojia kumetokea changamoto nyingi, moja wapo iliyo kuu kabisa ni kwamba lugha ya Kiswahili haimilikiwi na taifa lolote tajiri kwa hiyo katika harakatika za kuendeleza inakumbana na changamoto nyingi kama vile ukosefu wa fedha na hata utayari wa viongozi wa kisiasa kukiendeleza Kiswahili ni mdogo sana, hata hivyo harakati hizi zinapingwa na mataifa ambayo lugha zao zimeendelea sana kiteknolojia kwa kuhofia kwamba zitafunikwa na matumizi ya Kiswahili. Wapo tayari kutoa misaada ili kuendeleza lugha zao kukididimiza Kiswahili kitu ambacho kinafanya harakati za kukiendeleza Kiswahili kuwa ngumu kwani nchi kinamozungumzwa Kiswahili hazina pesa za kupambana na mataifa makubwa yanayopigia upatu lugha zao.
Kutokana na sababu hizo, kasi ya uundaji wa istilahi za kiteknolojia imekuwa ndogo sana, kwani kufanya hivyo pia kunahitaji pesa, na mara nyingi pesa zimekuwa zikitolewa na wahisani au makampuni yanayohusika kitu kinachotokea mara moja baada ya muda mrefu sana.
Pia, viongozi wa serikali hawajatilia mkazo suala hili, hawajaona umuhimu wa kukiendeleza Kiswahili kitenolojia. Nguvu zao nyingi wameziweka katika miradi mingine ya kimaendeleo huku wakisahau kabisa kuwa Kiswahili pia kinahitaji kwenda sambamba na maendeleo hayo. Kwa hiyo hii imekuwa ni changamoto katika maendeleo ya lugha ya Kiswahili.
Kwa kuwa istilahi hizi zimekuwa zikifanywa na watu tofautitofauti,  ni muhimu kuwapo na jopo maalumu la kusanifisha istilahi hizi kabla hazijasamabazwa. Kwa kufanya hivi hakutakuwa na matumizi tofauti ya istilahi katika dhana moja. Hali hii inajitokeza sana endapo uundaji wa istilahi utakuwa umefanywa katika makundi tofauti.
Utayari wa watumiaji; watumiaji wengi wa lugha ya Kiswahili wamekuwa wakilalamika kuhusu kutumia programu za komyuta kwa lugha za Kiswahili. Madai yao ni kwamba istilahi za Kiswahili ni ngumu sana na hivyo si rahisi kuzitumia, kwa mfano, wengi wamezoea kusema password na kwa hiyo ukiwaambi kwamba password kwa Kiswahili huitwa nywila au mouse inaitwa puku watabaki wakikushangaa na watona kama unawapa kazi kubwa sana. Kwa hiyo hii nayo inasabaisha matumizi ya Kiswahili katika vifaa vya kiteknolojia hususani kompyuta kuwa hafifu.
5.      Hitimisho
Katika makala hii tumeona TEHAMA ni kitu gani na umuhimu wake katika maisha ya kila siku ya binadamu, tumeona umuhimu wa lugha za kiafrika kuendelezwa katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa umahususi zaidi tumeona jinsi Kiswahili kilivyo muhimu zaidi katika uwanja wa maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Tumengalia pia maendeleo yaliyofikiwa na lugha ya Kiswahili katika TEHAMA huku tukionesha baadhi ya istilahi za Kiswahili zinazotumika katika matumizi ya kompyuta, pia tumeangalia changamotozinazo ikabili lugha ya Kiswahili katika jitihada za kuiendeleza kiteknolojia. Sasa tuangalie mapendekezo juu ya nini kifanyike ili kuhakikisha lugha ya Kiswahili inashika hatamu katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano:
Viongozi wa ukanda wa Afrika Mashariki waungane kuhakikisha wanaunda sera nzuri kuhusiana na maendeleo ya lugha ya Kiswahili ikiwa ni pamoja na kuandaa mradi maalumu wa kuunda istilahi mbalimbali za kiteknolojia, hii itasaidia lugha ya Kiswahili kuimarika katika matumizi ya teknolojia. Pamoja na hilo pia itenge bajeti maalumu kwa ajili ya kuandaa na kutekeleza miradi mbalimbali ya kuunda istilahi za Kiswahili katika teknolojia zinazoibuka ili kuahakikisha wazungumzaji wa lugha ya Kiswahili hawaachwi nyuma katika matumizi ya teknolojia mpya ziibukazo.
Pia kutokana na changamoto ya kutokuwapo na jopo maalumu la kuunda istilahi za kiteknolojia pindi mradi kama huu unapotokea, hali hii imesababisha kuwapo kwa istilahi ambazo hazijasanifishwa na pengine kuwapo na istilahi zaidi ya moja inayorejelea dhana moja, hii ni kwa sababu miradi kama hii hufanywa na watu tofautitofauti na pengine wataalamu hawa wana ujuzi katika lugha tu lakini katika teknolojia hususani kompyuta hawana maarifa ya kutosha au hawana kabisa. Katika hali kama hii ni vigumu kuunda istilahi zinazofanana au zinazobeba dhana kamili kama ilivyokuwa ikikusudiwa katika lugha chanzi. Kwa hiyo katika uundaji wa istilahi za kiteknolojia ni vema kuwepo na jopo maalumu amablo lina ujuzi wa kutosha katika lugha na masuala ya kiteknolojia, hii itasaidia kutoa istilahi nzuri na zinazoeleweka kwa urahisi kwa watumiaji.
Baada ya kuundwa istilahi hizi inatakiwa zisambazwe kwa watumiaji kwa kiwango kinachoridhisha ili waweze kujifunza na kuzifahamu na hatimaye kuzizoea katika matumizi yao ya kila siku katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Nasema hivi kwa saba usambazaji wa istilahi hizi umekuwa haufanywi kwa kiwango kinachohitajika, na katika usambazaji, vyombo vya habari vipewe kipaumbele, kwani istilahi hizi zikitumiwa na vyombo vya habari itakuwa rahisi sana kwa  watumiaji wengine kuzitumia.
Wazungumzaji wa Kiswahili pia wawe tayari kutumia istilahi hizi au programu za Kiswahili katika matumizi yao ya kopmyuta. Programu kadhaa za kompyuta zimejanibishwa kwa Kiswahili lakini wazungumzaji wengi wa Kiswahili bado wanatumia programu zilizoandikwa kwa lugha ya Kiingereza, program ya Windows 7 inapatikana kwa Kiswahili lakini nina wasiwasi kama miongoni mwetu kuna mtu hata mmoja anayetumia Windows 7 ya Kiswahili. Kwa hiyo napendekeza kwenu suala hili, kwa kuwa sisi tumejitoa kueneza na kuienzi lugha ya Kiswahili pia ni jukumu letu kuchangamkia fursa kama hizi, tuwe wa kwanza kutumia programu kama hizi kwa Kiswahili pindi zinapotokea, kwa kufanya hivi tutakuwa tunakienzi Kiswahili na kukikuza kwani  watu wanaotuzunguka watakapotuona tunatumia Windows ya Kiswahili watashawishika na wao kuitumia, hivyo kwa njia hii tutakuwa tumefanikiwa kukuza na kuienzi lugha ya Kiswahili.
Ninaamini kila mmoja  wetu ana ndoto za kuona lugha ya Kiswahili siku moja inakuwa lugha ya bara zima la Afrika, kwa maana kwamba Kiswahili kinazumgumzwa kila kona ya bara hili, basi kama ndio ndoto zetu sote hatuna budi kupigania maendeleo ya lugha ya Kiswahili kwa nguvu zetu zote, tukifanya hivi kwa pamoja kwa kijishughulisha na masuala yanayohusika na Kiswahili, kwa kuandika, kufanya utafiti katika Nyanja mbalimbali za lugha ya Kiswahili ndoto zetu zitatimia na kumbukumbu zetu zitakumbukwa katika vizazi vinavyokuja kama anavyokumbukwa leo hii Shaaban Robert. Ninaamini kuwa tunaweza!!
Kiswahili, Hazina ya Afika kwa Maendeleo Endelevu!

Marejeo
Akinyi, J.J. (2010). Kiswahili usage in ICT in NEPAD secondary schools in Kenya. Katika                                         TheJournal of Language, Technology & Entrepreneurship in Africa, Vol. 2. No.1.                             www.ajol.info/index.php/kcl/article/vieFile
Kahigi, K.K (2007). Ujanibishaji wa office na windows xp kwa Kiswahili sanifu. Katika  Kioo                           cha Lugha juzuu la 5. Dar es salaam. TUKI.
Kamau, S.N. (2009). Kiswahili, utandawazi na umoja wa Afrika. Katika journal of language, technology& entrepreneurship in Africa vol.1. www.ajol.info/index.php/kcl/article/vieFile
Katambi, S (2011). Teknolojia ya Habari na Mawasilianao (TEHAMA). Dar es salaam: Modecs                              Solutions
King’ei, K (2010). Misingi ya isimujamii. Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Msanjila,Y.P, Kihore,Y.M na D.P.B Massamba (2011). Isimujamii sekondari na vyuo.
                    Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Osborn, D. Z. (2006). African Languages and Information and Communication Technologies:                          Literacy, Access, and the Future. Katika  Selected Proceedings of the 35th Annual                   Conference on African Linguistics, ed. John Mugane et al., 86-93. Somerville, MA:                    Cascadilla Proceedings Project. www.lingref.com, document #1299.
Osborn, D. Z. (2010). African Languages in a Digital Age. Cape Town: HSRC Press.




CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM
 TAASISI YA TAALUMA ZA KISWAHILI
  IDARA YA LUGHA YA KISWAHILI  NA ISIMU


KI113:MBINU ZA UTAFITI  NA UANDISHI WA TASNIFU  KATIKA LUGHA NA FASIHI



RIPOTI YA UTAFITI KUHUSU  MBINU ZILIZOTUMIKA KATIKA UUNDAJI WA ISTILAHI ZA KISWAHILI ZILIZOINGIZWA KATIKA MIFUMO YA MAWASILIANO YA KOMPYUTA: MIFANO KUTOKA MFUMO WA KOMPYUTA WA LINUX.









JINA: MALAGIRA ARITAMBA.
NAMBA YA USAJILI: 2010-04-02466
MWALIMU WA SOMO: E. MAHENGE NA DKT. G. MRIKARIA


SHUKRANI
Utafiti huu umefanikiwa kwa jitihada kubwa za waalimu wangu wa somo.Napenda nimshukuru kwa dhati mwalimu Elizabeth Mahenge kwa kutumia muda wake mwingi  katika kunielekeza na kurekebisha mada yangu ya utafiti.Namshukuru pia Mwalimu G.Mrikaria kwa kututia moyo katika kufanikisha utafiti huu.
Vilevile nawashukuru wanafunzi wenzangu kwa kunishauri na kunitia moyo katika kuendelea na utafiti huu.Wanafunzi wafuatao wamekuwa mchango mkubwa katika kufanikisha utafiti huu;Ally Laila,Thomas Edson,Ndumbaro Eric, Ndege Busalu pamoja na Ntenga Elias.Nawashukuru pia Boniface Jacob na James Balele kwa utayari wao wa kunisaidia kuchapa utafiti huu.Na mwisho nawashukuru wote walionisaidia kwa namna moja ama nyingine,Mungu awabariki sana!

.  












                                                                          
                                               YALIYOMO
Sura ya kwanza:Utangulizi na Nadharia ya uundaji istilahi…………………. 1
1.0  Utangulizi……………………………………………………………………………………1
1.1  Tatizo la utafiti……………………………………………………………………….3
1.2  Malengo ya utafiti…………………………………………………………………....3
1.3  Umuhimu wa utafiti…………………………………………………………………4
1.4  Dhana ya istilahi,linux na nadharia ya uundaji istilahi……………………………4
Sura ya pili:Mapitio ya marejeo na mbinu za ukusanyaji data………………..8
2.1 Mapitio ya marejeo………………………………………………………………………….8
      2.2 Mbinuza ukusanyaji data ……………………………………………………………..10
Sura ya tatu:Uchambuzi wa data………………………………………………11
3.1 Utangulizi………………………………………………………………………………….11
       3.2 Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika Linux………….11
       3.3 Ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika kuunda istilahi za Kiswahili katka Linux…16
             3.3.1 Ubora wa mbinu zilizotumika ……………………………………………………16
             3.3.2 Udhaifu wa mbinu zilizotumika…………………………………………………18
             3.3.3 Mbinu bora zaidi katika uundaji wa istilahi za Kiswahili…………………………19
Sura ya nne:Muhtasari na Hitimisho…………………………………………..20
4.1 Matokeo ya utafiti kwa muhtasari…………………………………………………………20
4.2 Hitimisho…………………………………………………………………………………….22
Marejeo
Viambatisho  
                                      
                                       SURA YA KWANZA
1.0   Utangulizi
Lugha ni kielelezo cha maisha ya jamii kwani huenda sambamba na mabadiliko au maendeleo katika jamii. Kila sekta ya jamii iwe  siasa,elimu,sayansi,teknolojia,utamaduni,dini,kilimo,uhandisi,sanaa,uchumi ama biashara hubadilika kila mara .Uvumbuzi mpya kila mara huzua dhana mpya ambazo zinahitaji maneno mapya kuzielezea(King’ei 2010)
King’ei(ameshatajwa) anaendelea kusema kuwa  ukuzaji wa msamiati na istilahi ni jambo la kawaida katika kurekebisha lugha ili iweze kuambatana na wakati au iwe ya kisasa. King’ei anaendelea kusema kuwa ukuzaji upya wa istilahi hufanyika kwa sababu mbalimbali.Kwanza kabisa lugha sharti iweze kuelezea dhana mpya zinazoingia katika jamii kutokana na mabadiliko katika jamii.Sababu ya pili ni kwamba maana ya maneno yanayotumika katika lugha hupanuliwa ili kuchukua maana mpya au pana kuliko ile ya awali.Sababu ya tatu ya kuwepo haja ya kustawisha istilahi mpya katika lugha ni ile haja ya kufasiri maandishi kutoka lugha moja hadi nyingine.
Msanjila na wenzake (2011) wanasema hadi wakati huu lugha ya Kiswahili imekwisha ingizwa katika mifumo miwili ya kompyuta ijulikanayo kama linuksi na mikrosofti.Wanaendelea kusema,kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo hii maana yake ni kwamba mtumiaji anaweza kuvinjari mifumo hiyo ya kompyuta kwa Kiswahili akiamua kufanya hivyo.
Pia King’ei(ameshatajwa) anaelezea kuwa,kampuni ya talakirishi iitwayo microsoft ilitekeleza hatua ya kihistoria  mwaka 2005 kwa kuanzisha kamusi maalumu inayo wawezesha watumiaji wa talakirishi kutumia lugha ya Kiswahili katika mawasiliano yao yote kwa kompyuta,anaendelea kusema,programu hii mpya inamwezesha mtumiaji kompyuta asiyefahamu lugha nyingine kama vile kiingereza kutumia kompyuta na kuwasiliana bila shida yoyote.
Katika mchakato wa kuziweka programu hizi katika Kiswahili, ilihitajika kuunda istilahi za

Kiswahili ili kukamilisha shughuli hii mbinu mbalimbali za uundaji istilahi zilitumika.
Katika uundaji wa istilahi za Kiswahili kuna mbinu mbalimbali zinazotumika. Kwa mujibu wa
Kiango(2004) amebainisha mbinu za kuunda istilahi za Kiswahili kuwa ni pamoja na:Kubuni,anasema,njia hii inaweza kutumika katika kukabili mazigira ya aina mbili; kubuni msamiati ambao utataja mambo yaliyomo katika jamii ambayo hayajapata msamiati wa Kiswahili. Pili ni kubuni msamiati ambao utataja mambo kutoka nje ya jamii yenye msamiati wa kigeni, mbinu nyigine ni kukopa; kukopa kwa kutohoa msamiati wa kigeni,kukopa kwa kutafsiri msamiati wa kigeni na kukopa kwa kuingiza maneno ya kibantu na lahaja na njia nyingine ni ya kufupisha maneno.
Kahigi (2004) anasema mbinu  za kuunda istilahi ni pamoja na: unyambulishaji; unyambulishaji ni kupachika viambishi undaji ili kuunda neno lenye dhana na muafaka. Mfano, modification→ukumushaji. Mbinu nyigine ni ukopaji; ukopaji ni kuchukua neno kutoka lugha chanzi na kulitohoa ili likubaliane na taratibu za kisarufi za lugha pokezi. Mbinu zingine zilizoainishwa na Kahigi ni: tafsiri mkopo;ni aina ya tafsiri kutoka lugha chanzi ambayo ni ya moja kwa moja, mbinu nyigine ni uundaji wa maneno mapya, mbinu hii huhusisha uundaji wa maneno mapya ambayo yalikuwa hayapo kwenye lugha lengwa, mfano byte  >  baiti, uambatani; ni uwekaji wa maneno mawili au zaidi yanayowakilisha dhana moja, mfano magneticfield >ugasumaku, ufupishaji; hii ni mbinu ya kufinyanza maneno na kupata neno moja, mfano, UWT(Umoja wa Wanawake Tanzania).
Mtafiti mwingine ambaye ameelezea mbinu za uundaji istilahi ni Sewangi(2004) yeye anasema mbinu za uundaji istilahi ni pamoja na: kutohoa,kwa mfano; computer > kompyuta, program>programu, mbinu nyingine ni kubuni, kwa mujibu wa Sewangi anasema, mbinu ya kubuni inaweza kufanywa kidhahania au kwa kutumia vigezo mahususi. Kubuni istilahi   kidhahania  hutetewa kwa hoja kuwa hakuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya istilahi na dhana inayo bebwa, hivyo neno lolote laweza kuundwa na kupewa hadhi ya istilahi ya dhana fulani. Njia mojawapo ya kuunda istilahi kidhahania ni kutumia fomula za kompyuta ambapo maneno mengi yanaweza kuzalishwa na kupachikwa dhana mahususi katika uwanja fulani wa maarifa. Njia ya kuunda istilahi kivigezo huweza kufanywa kwa kutumia vigezo mahususi kama

vile kazi, umbo au mwonekano wa kitu. Kwa mfano kwa kutumia kigezo cha kikazi kisawe cha calculator kimebuniwa kuwa ni kikokotozi (kitu kinachofanya kazi ya kukokotoa), kisawe cha data saver kimekuwa kihifadhi data (kitu kinachohifadhi data). Mbinu nyingine iliyoainishwa na Sewangi ni mbinu ya kupanua maana ya maneno yaliyopo; njia hii huchukua neno lenye maana ya jumla na kuliongezea maana ya kihistilahi katika mazingira ya kitaalamu, kwa mfano neno kifaru ambalo maana yake ya jumla ni mnyama lakini katika mazingira ya utaalamu wa kijeshi ni kisawe cha tank.
Kwa kuzingatia maelezo ya wataalamu hawa kuna mbinu tofautitofauti za kuunda istilahi. Kwa hiyo kutokana na kwaba kuna mbinu tofautitofauti za kuunda istilahi,utafiti huu hulenga kubainisha mbinu zilizotumika katika kuunda istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika mfumo wa kompyuta wa linux.

1.1 Tatizo la utafiti
Kulingana na tafiti za wataalamu hawa,wameelezea kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo ya kompyuta ya linux na Microsoft,kwa mfano, Msanjila na wenzake (2011) na King’ei (2010) wameelezea kuhusu hili. Vilevile wataalamu wengine kama vile Kiango (2004), Sewangi (2004) na Kahig i(2004) wao wameainisha mbinu mbalimbali za kuunda istilahi za Kiswahili. Kwa ujumla wataalamu hawa hawajaonyesha mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika mifumo ya mawasiliano ya kompyuta hususani mfumo wa kompyuta wa linux, kwa hiyo utafiti huu hulenga kuziba pengo hili kwa kuchunguza mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux.
1.2 Malengo ya utafiti
Malengo ya utafiti huu yamegawanyika katika sehemu kuu mbili:
1.2.1 Lengo kuu na
1.2.2 Malengo mahususi

1.2.1 Lengo kuu
Lengo kuu la utafiti huu ni kutaka kutalii istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika mfumo wa mawasiliano ya kompyuta wa linux na kuainisha mbinu zilizotumika kuunda istilahi hizo.
1.2.2 Malengo mahususi
Malengo mahususi ya utafiti huu ni mawili, ambayo ni: kupambanua ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili  katika linux na kubainisha mbinu bora zaidi inayoweza kutumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili.
1.3 Umuhimu wa utafiti
Umuhimu wa utafiti huu ni kwamba utasaidia kubainisha mbinu bora za uundaji wa istilahi za Kiswahili. Vilevile utafiti huu utawasaidia watumiaji wa kompyuta wanaotumia programu hii ya linux kwa Kiswahili kuelewa kwa urahisi istilahi zilizotumika baada ya kubainisha mbinu zilizotumika katika kuunda istilahi hizo.
1.4 Dhana ya istilahi, linux na nadharia ya uundaji istilahi
Istilahi ni dhana iliyofasiliwa na wataalamu mbalimbali na wote wanakubaliana kuwa, istilahi ni msamiati utumikao katika uwanja fulani maalumu wa lugha. Wataalamu wanaokubaliana na fasili hii ni pamoja na King’ei(2010), Samson(1988) na Kiango(2004). Kwa hiyo kulingana na fasili hii si kila msamiati ni istilahi bali msamiati huwa istilahi pale unapotumika katika Nyanja maalumu za kitaaluma. Kila uwanja maalumu wa kitaaluma huwa na msamiati wake ambao hauna maana nje ya taaluma hiyo wala haufahamiki kwa wazungumzaji lugha wasiokuwa wataalamu wa lugha hiyo. Kwa mfano msamiti unaotumika katika isimu,fasihi,teknolojia ya habari na mawasiliano na kadhalika ni maalumu na hutumiwa na kueleweka tu na wataalamu wahusikao na nyaja husika.
Linux kwa mujibu wa Msanjila na wenzake(2011) ni mfumo wa kompyuta huria unao ruhusu watu mbalimbali kuchangia katika marekebisho na maendeleo yake. Kimsingi linux ni mfumo endeshi wa kompyuta. Ni program katika kompyuta iayosaidia programu-tumizi na mtumiaji wa kompyuta kufikia vifaa fulani katika kompyuta ili kufanya kazi iliyokusudiwa, linux ni sawa na

program-tumizi zingine kama vile windows (Linux.com).
Nadharia ya uundaji istilahi hujumuisha mambo kadhaa, kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko(2008) mambo hayo ni pamoja na sababu za uundaji wa istilahi, njia au mbinu za uundaji istilahi,vyombo vya uundaji istilahi na misingi ya uundaji istilahi.
Katika sababu ya uundaji istilahi Tumbo-Masabo na Mwansoko wanasema kuwa, uundji wa istilahi ni muhimu panapotokea haja ya kushughulikia nyanja ambazo zilikuwa hazishughulikiwi kwa kutumia lugha fulani. Uundaji huo aghalabu hufanywa ili kukidhi haja ya mawasiliano katika elimu ya juu, ufundi na utaalamu,na shughuli zinazohusu serikali na teknolojia. Kwa hiyo nadharia ya uundaji istilahi huambatana na sababu au haja fulani ya kufanya hivyo. Kwa mfano uundaji wa istilahi za Kiswahili katika mfumo wa kompyuta wa linux umeambatana na sababu kwamba, kuuweka mfumo huu  wa kompyuta katika Kiswahili ili kusudi watumiaji wa Kiswahili waweze kuutumia mfumo huu kwa lugha wanayo ifahamu.
Vyombo vinavyohusika katika uundaji wa istilahi.
Katika kutekeleza kazi ya kuunda istilahi vimewekwa vyombo maalumu vinavyo tekeleza suala hili, kwa mfano Tanzania chombo kilchopewa jukumu hili na serikali ni Barza la Kiswahili la Taifa (BAKITA).
Vilevile katika nadharia ya misingi ya uundaji istilahi huzingatia mambo yafuatayo:
·         Uundaji wa istilahi ni budi uanzie kwenye dhana.
·         Dhana hizo zieleweke kwa ukamilifu na uwazi.
·         Uhusiano baina ya dhana ndio uwe msingi wa uundaji wa istilahi, istilahi kopwa zichukuliwe kama zilivyo katika umbo lake la asili kwa kufanya marekebisho machache tu kulingana na sarufi na matamshi ya lugha kopaji.
·         Istilahi inafaa ziwe fupi iwezekanavyo lakini zieleweke.
·         Istilahi ziwe na muundo unaoeleweka yaani zifuate mofolojia ya lugha.
·         Uundaji wa istilahi kwa vifupisho na akronomia uepukwe hasa kama istilahi kamili si ndefu sana.
·         Istilahi zisiwe na sinonimia au homonimia.
·         Istilahi ziundwe kwa njia ambayo itakuwa rahisi kuunda istilahi nyingine kwa

mnyambuliko.
·         Istilahi zitolewe kufuatana na mfumo wa dhana yaani ziainishwe kuliko kuandikwa kwa alfabeti.
·         Muundo wa istilahi udokeze maana yake kwa watumiaji wa lugha husika. Kwa hiyo misingi hii haina budi kufuatwa katika mchakato wa uundaji istilahi.
Nadharia nyingine kama ilivyoainishwa na Tumbo-Masabo na Mwansoko(wameshatajwa) ni njia za uundaji istilahi. Katika uundaji wa istilahi kuna njia kuu mbili ambazo zinatumika zaidi, njia hizo ni pamoja na:
(i)                 Kutafsiri hasa kutoka kwenye lugha zinazojulikana kuwa ni za kimataifa kama vile Kifaransa, Kiingereza, Kihisipania.
(ii)               Kuunda istilahi kutokana na mifumo ya dhana.
Njia ya kutafsiri hutumiwa sana na vyombo vingi vya uundaji istilahi kinyume na misingi ya uundaji ambayo inasisitiza kuwa uundaji huo uanze na dhana, msingi wa njia hii ni istilahi za lugha chasili ambazo aghalabu hupangwa kwa alfabeti. Faida ya njia hii ni kwamba istilahi nyingi zinaweza kushughulikiwa  kwa muda mfupi pia istilahi za lugha lengwa huweza kutafsiriwa katika lugha za kimataifa. Hata hivyo hasara ya njia hii ni kwamba kwa vile kila istilahi hushughulikiwa peke yake, hali hii huweza kusababisha mtiririko wa mfumo wa istilahi usio na ulingano.
Kahigi (2004) anasema kuunda istilahi kutokana na mifumo ya kidhana ni kwamba istilahi huundwa kufuatana na mifumo hiyo. Kwa mfano katika hisabati kuna mifumo ya elimu-maumbo, elimu-namba, vipimo na kadhalika. Mathalani katika kuunda istilahi za dhana ya pembe itabidi dhana zifuatazo zishughulikiwe zote kwa pamoja: pembekali, pembenukta, pembetatu, pembemshabaha, pebemstari na kadhalika. Faida ya mkabala huu ni kwamba mwishowe mifumo yote ya dhana huwa na mtiririko wenye ulingano.
Katika nadharia hii ya njia za uundaji istilahi mbinu mbalimbali hutumika, mbinu hizo ni pamoja na:mwabatano; hii ninjia ya uundaji istilahi kwa kuambatanisha maneno mawili au zaidi yaliyo 
huru. Mfano ; mbwa kichaa.
Mnyambuliko;ni uundaji wa neno jipya kwa kuambatisha viambishi kewenye mzizi au shina la neno. Mfano;wekeza  >  uwekezaji.
Muungano; hii mbinu ni sawa na mwambatano isipokuwa katika muungano maneno mawili au zaidi huunganishwa ili kuunda neno moja, mfano;kiini+macho  >  kiinimacho.
Kupanua maana ya maneno; huu ni mchakato ambapo neno lililopo kwenye lugha hupewa maana pana zaidi ya maana yake ya awali. Mfano butu maana yake ya kawaida ni –sio kali,-sio kata. Maana ya kihistilahi ni pembe ambayo ni zaidi ya nyuzi 90 na ndogo kuliko nhyuzi180(hisabati).
Ufupisaji; ni mbinu ambayo inatumika kufinyanza fungu la maneno ili kuunda neno moja,mfano; BAKITA (Baraza la Kiswahili laTaifa).
Ukopaji; ni matumizi ya neno kutoka lahaja ama lugha nyingine, aghalabu neno hilo hubadilishwa ili lishabihi muundo wa lugha lengwa.
Tafsiri-sisisi; ni aina ya tafsiri kutoka lugha chasili ambayo ni ya moja kwa moja. Mfasiri habadili lolote ila anahakikisha tu tafsiri inakuwa sahihi kwa mujibu wa lugha lengwa. Kwa hiyo katika mchakato wa uundaji wa istilahi za Kiswahili mbinu hizi hutumika.








                                                        
SURA YA PILI 
  Mapitio ya marejeo na mbinu za utafiti.
2.1 Mapitio ya Marejeo
Kutokana na mabadiliko yanayotokea katika jamii wataalamu wameonesha umuhimu wa lugha kuyakabili mabadiliko hayo. King’ei(2010) anasema lugha ni kielelezo cha maisha ya jamii siasa, elimu, sayansi, teknolojia, utamaduni, dini, kilimo, uhandisi, sanaa, uchumi ama biashara hubadilika kila mara, uvumbuzi mpya kila mara huzua dhana mpya ambazo zinahitaji maneno mapya ya kuzielezea.
Kulingana na kukua kwa teknolojia ya habari na mawasiliano,lugha ya Kiswahili haina budi kuyakabili mazingira haya. King’ei(ameshatajwa) anaelezea hatua ya kihistoria iliyochukuliwa na kampuni ya Microsoft mwaka 2005 kwa kuanzisha kamusi maalumu inayowawezesha watumiaji wa kompyuta kutumia lugha ya Kiswahili katika mawasiliano yao yote kwa kompyuta. Kwa maana kwamba katika programu hii mpya inamwezesha mtumiaji kompyuta asiyefahamu lugha nyingine kama vile kiingereza, kutumia kompyuta na kuwasiliana bila shida yoyote kwa Kiswahili.
Mtafiti mwingine ni Msanjila na wenzake(2011) wanasema hadi wakati huu lugha ya Kiswahili imekwisha ingizwa kwenye mifumo miwili ya kompyuta ijulikanayo kama linuksi na mikrosofti. Wanaendelea kusema kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo hii maana yake ni kwamba mtumiaji anaweza kuvinjari mifumo hiyo ya kompyuta kwa Kiswahili akiamua kufanya hivyo.
Kimsingi hatua ya kuingiza Kiswahili katika mifumo hii ya kompyuta ni hatua muhimu sana katika maendeleo ya teknolojia ya habari na mawasiliano, katika mchakato wa kuiweka mifumo hii katika lugha ya Kiswahili ilihitajika kuundwa istilahi za Kiswahili ili mifumo hii iwekwe katika Kiswahili. Katika kuunda istilahi za Kiswahili mbinu mbalimbali hutumika, wataamu mbalimbali wamejadili kuhusu mbinu hizo:
Tumbo-Masabo na Mwansoko(2008) wanasema mbinu za uundaji istilahi ni pamoja na: Muungano wa maneno, mfano; mwanaisimu, mwambatano wa maneno, mfano; nusu kipenyo,
8
Unyambulishaji, mfano; ambisha  >  uambishaji, upanuzi wa maana za maneno, uhulutishji, mfano; kizigeu  >  kiziogeu, ukopaji (kukopa kutoka lugha za kigeni, lugha za kibantu au lahaja) na tafsiri-sisisi (tafsiri mkopo), mfano; measure of time  >  kipimo cha wakati.
King’ei(2010) ameainisha mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili kuwa ni pamoja na uunganishaji wa maneno, ukopaji, kutafsiri maneno ya kigeni, mbinu ya ufupishaji mfano;UKIMWI (Upungufu wa Kinga Mwilini) na utohozi.
Kahigi (2004) anasema mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili ni pamoja na:unyambulishi, uambatani, uhulutishi, ufupishaji, utemaji, ukopaji, tafsiri mkopo na uundaji wa maneno mapya kabisa.
Vilevile Kiango (2004) ameanisha mbinu zifuatazo katika undaji wa istilahi za Kiswahili: kubuni na kukopa (kutoka lugha za kigeni, lugha za kibantu na lahaja).
Kwa hiyo kulingana na wataalamu hawa tunaweza kuanisha mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili kuwa ni:
·         Unyambulishji   
·         Muungano wa maneno
·         Mwambatano wa maneno
·         Ukopaji
·         Tafsiri mkopo(tafsiri sisisi)
·         Uhulutishaji
·         Ufipishaji
·         Utemaji
·         Upanuaji wa maana ya maneno yaliyopo na
·         Kubuni
Tafiti za wataalamu hawa zina umuhimu mkubwa kwani zimesaidia kujua kuingizwa kwa Kiswahili katika mifumo ya kompyuta ya linux na Microsoft na vilevi zimetusaidia kujua mbinu za uundji istilahi za Kiswahili. Kwa hiyo katika utafiti wetu tutabainisha mbinu zilizotumika

kuunda istilahi za Kiswahili katika linux kati ya hizo zilizoainishwa na wataalamu hao
2.2 Mbinu za ukusanyaji data
Katika utafiti huu mbinu iliyotumika ni moja, yaani mbinu ya kusoma marejeo mbalimbali hii ni kwa kuwa utafiti huu ni wa kimakitaba. Mbinu hii imetumika katika ukusanyaji wa data zinazohusu istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika mfumo wa kompyuta wa linux, ambapo mbinu  hii imetumika kwa kusoma marejeo kwa njia ya wavuti na kukusanya istilahi za Kiswahili zilizokuwepo katika mfumo wa kompyuta wa linux.
Mbinu hii pia imetumika katika kukusanya data zinazohusu mbinu za uundaji istilahi za Kiswahili. Kwa kusoma marejeo mbalimbali data zinazohusu mbinu za uundaji wa istilahi za Kiswahili zilikusanywa.
Vilevile mbinu hii imetumika katika ukusanyaji wa data zinazohusu ubora na udhaifu na udhaifu wa mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux. Na pia mbinu hii imetumika katika ukusanyaji wa data zinazohusu kubainisha mbinu bora katika kuunda istilahi za Kiswahili.
Data katika utafiti huu zimekusanywa kutoka faharasa ya teknolojia ya habari ya KILinux(KlnX) juzuu ya kwanza. Faharasa hii inajumuisha orodha ya istilahi 700. Sampuli ya utafiti huu inajumuisha istilahi 100. Sampuli hii imechukuliwa kinasibu (kiholela) yaani hakuna mpangilo au utaratibu wowote maalumu uliofutwa katika uchukuaji wa sampuli.



                                            


SURA YA TATU
Uchambuzi wa data
2.1 Utangulizi
Utafiti huu umegawanyika katika sehemu kuu mbili, sehemu ya kwanza inahusu  uchambuzi wa data zinazohusu mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux na sehemu ya pili inahusu kupambanua ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika kuunda istilahi za Kiswahili katika linux na kubainisha mbinu iliyo bora katika kuunda istilahi za Kiswahili. Katika uchambuzi wa data hizi tutatumia nadharia ya uundaji istilahi za Kiswahili ambayo imekwishaongelewa katika kipengele cha 1.4.    
2.2  Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika linux.
Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux ni kama zilivyobainishwa hapa chini:
Unyambulishi; katika mbinu hii kitenzi kinaweza kugeuzwa kikawa nomino au kivumishi kinaweza kugeuzwa kikawa kitenzi au au nomino. Mbinu hii imetumika kwa kiasi kikubwa, mifano ifuatayo hudhihirisha matumizi ya mbinu hii.
·         Accessing   >   ufikio ( viambishi u-i-o vimeambatiswa katika shina fika).
·         Accsess     >      fikio (viambishi i-o vimenyambulishwa katika shina  fika )
·         Allocation    >     utengaji (viambishi u-aji vimeambatishwa katika shina tenga)
·         Bookmark link   >   alamisho (viambishi ish-o vimeambatishwa katika shina alama).
·         Bookmark   >   alamisha(t) (viambishi ish-a vimeambatishwa na kuunda kitezi alamisha)
·         Deleting    >   ufutaji (viambishi u-aji vimeambatishwa katika kitenzi futa  )
·         Deletion    >    mfuto (viambishi m-o vimeambishwa katika kitenzi futa nakupata neno                                         mfuto)
·         Input   >    ingizo (kiambishi –o kimeambishwa katika shina ingiza na kuunda istilahi ingizo).

·         Interactive   >   wasilianifu ( kiambishi –ifu kimeambishwa katika shina wasiliana na kuunda neno wasilianifu).
·         Allocation(n)   >    mtengo (viambishi m-o vimeambishwa katika shina tenga na kuunda nomino mtengo ikiwa na dhana ya matokeo).
Mwabatano; hii ni njia inayotumika kwa kuambatanisha maneno mawili au zaidi. Katika linux kuna istilahi zenye mwambatano wa maneno mawili na mwambatano wa maneno matatu. Mifano ifuatayo inadhihirisha matumizi ya mbinu hii:
·         Add-on help   >   msaada nyongeza ( yameambatishwa maneno msaada na nyongeza).
·         Alphabet text character   >   kiwambo alfabeti (kiwambo + alfabeti).
·         Aperture value   >    thamani upenyo (thamani + upenyo)
·         Background colour    >   rangi usuli (rangi + usuli).
·         Block device    >     kitunza data ( (ki)tunza + data).
·         Bullet list   >    orodha tobwe (orodha + tobwe).
·         Composer    >    programu tumizi (programu+ tumizi).
·         Configuration utility   >   programu sanidi (programu + sanidi).
·         Checksum    >    namba thibitishi (namba + thibitishi).
·         Encrypted    >    msimbo fiche (msimbo + fiche).
Vilevile kuna istilahi zilizoundwa kwa kuambatanisha maneno matatu. Mfano:
·         Encrypted text   >   matini-msimbo fiche (matini + msimbo + fiche).
·         Full-screen mode   >   modi-skrini nzima (modi + skrini + nzima).
·         Small caps   >      herufi kubwa ndogo (herufi + kubwa + ndogo)
·         Column spam   >    upana-safu wima (upana + safu + wima).
·         Default search engine   >   injini tafuti-msingi (injini + tafuti + msingi).
·         Com port (communication port) >  mlango wa mawasiliano(mlango+wa+mawasiliano).
Muungano; hii ni mbinu ya kuunganisha maneno mawili au zaidi ili kupata neno moja mbinu hii pia imetumika kuunda istilahi za Kiswahili katika linux. Mifano ifuatayo inabainisha

kutumika kwa mbinu hii:
·         Anonymity   >   ufichojina (uficho + jina).
·         Arccosine   >    kosinitao (kosini + tao).
·         Backslashes   >   mkwajunyuma ( mkwaju + nyuma).
·         Data area    >    eneodata (eneo + data).
·         Data bank   >    kanzidata (kanzi + data).
·         Data base    >    kihifadhidata ( (ki)hifadhi + data).
·         Footnote    >    tiniwayo (tini + wayo).
·         Hypertext   >   matinifora (matini + fora).
·         Keybody    >    baobonye (bao + bonye).
·         Newsgroup   >   kundihabari (kundi + habari).
·         Spreadsheet   >   lahajedwari (laha + jedwari).
Ukopaji; njia hii pia imetumika kuunda isuilahi za Kiswahili katika linux. Mifano ifuatayo inaonyesha kutumika kwa mbinu hii.
·         Account    >    akaunti
·         Adapter    >   adapta  
·         Ampersand   > ampasendi
·         Applet   >    apuleti
·         Autoformat   >    fomati otomati
·         Baud   >       baudi
·         Boolean   >    buleani
·         Buffer    >     bafa
·         Cursor    >     kasa
·         Daemon    >   dimoni
·         Dial    >     dayo
·         Digit    >   dijiti
·         Icon    >    ikon
·         Kilobyte    >    kilobaiti

·         Pixels    >     pisel
·         Printer   >  printa
Mbinu hii ya ukopaji imetumika kwa kiasi kikubwa katika uundaji wa istilahi za Kiswahili zilizopo katika linux.
Mbinu nyingine iliyotumika kwa kiasi kikubwa katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux ni mbinu ya tafsiri mkopo (tafsiri sisisi). Tafsiri mkopo nitafsiri ya moja kwa moja kutoka lugha chanzi. Mifano ifuatayo inathibitisha matumizi ya mbinu hii katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux.
·         Actions menu   >   menyu vitendo.
·         Address book   >   kitabu cha anwani.
·         Alert me    >     nitahadharishe.
·         Auto complete     > kamilisha kiotomati.
·         Boolean operations     >     matendo buleani.
·         Certificate manager    >    meneja ithibati.
·         Certificate viewer      >     kionyeshi hati.
·         Chat group    >     kundi sogozi.
·         Colour capability    >     uwezo kirangi.
·         Connection failure     >     unganisho shinde.
·         Control panel     >    paneli dhibiti.
·         Country code    >     msimbo nchi.
·         Device manager    >    meneja vifaa.
·         Dialogue box     >     kisanduku cha mawasiliano.
·         Drag and drop   >    kokota na dondosha.
·         Eject     >       fyatua.
·         Flow control     >     udhibiti wa mtiririko.
·         Word processor    >    kichakata matini.
·         Web master    >     mtawala tovuti.

Mbinu nyingine ni mbinu ya kuunda maneno mapya kabisa mbinu hii imetawaliwa na maneno ya mkopo. Mfano:
·         Icon   >     ikoni
·         Italic    >   italiki
·         Label    >   lebo
·         Megabyte(MB)   >    megabaiti(MB)
·         Menu proxies    >    menyu proksi
·         Manager   >    meneja
·         Pixels   >     piseli
·         Program    >   programu
·         Scan    >    skani.
·         Scanner    >  skana
·         Tab    >    tabo
·         Tag    >  tagi
Mbinu ya ufupishaji pia imetumika katika kuunda istilahi za Kiswahili katika linux; hii ni mbinu inayotumika kufinyanza fungu la maneno na kupata neno moja. Mifano ifuatayo huonyesha matumizi ya mbinu hii:
·         Alt(alternate)    >    Kbdl (kibadala)
·         BSS (Bulletin Board Service)     >     HUM (Huduma za Ubao wa Matngazo)
·         Ctrl (ontrol)     >   Kdbt (kidhibiti)
·         ESC (escape)   >    Epa (epuka)
·         FAQ (frequently asked quetions)   >    MYM (Maswali Yaulizwayo Mara kwa mara)
·         FTP (file transfer protocol)    >      IKF (Itifaki ya Kuhawalisha Faili)
·         FYI (For Your Information)    >    KTY (Kwa Taarifa Yako)
·         Megabyte (MB)       >      megabaiti (MB)
·         Ref:           >       Yah:
·         Re:             >        Jb:
·         TCP (Transfer Control Protocol)      >     IKU (Itifaki ya Kudhibiti Urushaji)

·         URL (Uniform Resource Location)   >   KISARA (Kioneshi Sanifu Rasilimali)
·         WWW (World Wide Web)      >    WWW (Wavu Wa Walimwengu)
Uhulutishi ni mbinu pia liyotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux, mbinu hii hutumika katika uundaji wa istilahi kwa kuunganisha sehemu za maneno na kuunda neno moja. Mbinu hii imetumika kwa kiasi kidogo sana, rejea mifano ifuatayo:
·         Bitmap    >   taswidoti ( (taswi)ra + doti)
·         Multimedia    >   medianuwai ((medi)a + anuwai)
Mbinu nyingine iliyotumika katika uundaji wa istilahi za kiswahili katika linux lakini kwa kiasi kidogo sana ni ile mbinu ya upanuzi wa maana za maneno, upanuzi wa maana za maneno ni kuongezea maana maalumu za kihistilahi katika maneno ya Kiswahili. Mfano:
·         Mouse      >       puku
Puku kwa maana ya kawaida ni panya pori lakini hapa limepewa dhana mahususi katika kompyuta kwa maana ya kifaa kinachotumika katika utumiaji wa kompyuta.
Utemaji (clipping) ni mbinu pia iliyojitokeza kwa kiasi kidogo sana, kwa kutumia mbinu hii istilahi huundwa kwa kukata sehemu ya neno na sehemu ya neno itakayobaki hutumika kama istilahi. Mfano: key (on keyboard)     >    kibonye ( kutoka neno bonyeza na kuongeza kiambishi cha ngeli ya saba ki-).
Kwa hiyo hizi ndizo mbinu zilizobainika kutumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili zilizoingizwa katika mfumo wa kompyuta wa linux.
2.3 Ubora na udhaifu wa mbinu zilizotumika kuunda istilahi za Kiswahili katika linux.
2.3.1 Ubora wa mbinu zilizotumika.
Kwa kiwango kikubwa mbinu zilizotumika zimezingatia misingi na kanuni za uundaji istilahi. Kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko (2008) wanabainisha kuwa misingi mahususi

katika uundaji wa istilahi ni pamoja na: Uangavu wa wa istilahi iliyoundwa yaani istilahi ziakisi sifa bainifu za dhana zinazoziwakilisha. Mbinu zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux kwa kiasi kikubwa zimezingatia msingi huu. Kwa mfano:
Ufikio     >    accessing,         ingizo    >     input,   alamisha     >     bookmark.
Istilahi hizi zinaonyesha wazi dhana zinazowakilishwa, kwa mfano, alamisha inabeba dhana ya   kitendo cha kuweka alama hivyo kwa msingi huu inadhihirisha mbinu zilzotumika ni bora. Vilevile mbinu zilizotumika zimezingatia msingi wa uundaji istilahi unaosema, istilahi sharti ziwe na uwezo mkubwa wa kunyambuliwa na kuunda istilahi nyingine za kikoa au ukanda unaohusika. Msingi huu umefuatwa katika kuunda istilahi za kwenye linux, kwani istilahi nyingi zilizoundwa zina uwezo wa kunyambulishwa. Mfano:
·         Add   >    ongeza
·         Add-on    >    nyongeza
·         Alert(n)    >    thadhari
·         Alert(v)     >    tahadharisha
Pia uundaji wa istilahi za kwenye linux umezingatia msingi wa uundaji istilahi unaosema,uwakilishi wa istilahi moja kwa dhana moja. Msingi huu umezingatiwa kwa kiasi kikubwa kwani istilahi takribani zote huwakilisha dhana moja isipokuwa zile zilizoundwa kwa kupanua maana ambazo ni chache sana.
Mfano: configuration    >  usanidi
             Configuration file   >   faili sanidi
Vilevile mbinu zilizotumika ni bora kwani hazijatumia kwa kiasi kikubwa mbinu za uhulutishi na mbinu ya kupanua maana ya maneno yaliyopo, hii ni kwa sababu misingi ya uundaji wa istilahi za Kiswahili husisitiza kuepuka matumizi ya mbinu hizi; hii ni kwa kuwa istilahi zinazo uundwa kwa mbinu ya uhulutishi huwa na uvulivuli wa maana na kufanya kuwa ngumu kukumbukwa na kutumiwa. Pia uundaji wa istilahi kwa kupanua maana ya maneno yaliyopo husababisha watumiaji wa istilahi hizi kushindwa kutofautisha maana zake za kawaida na zile za

kihistilahi.
Mbinu za uundaji istilahi za Kiswahili katika linux, pia zimezingatia msingi wa uundaji wa istilahi za Kiswahili unaosema, istilahi sharti ziwe fupi na zenye kueleweka. Istilahi nyingi zimeundwa kwa kuzingatia msingi huu.

2.3.2 Udhaifu wa mbinu zilizotumika
Katika uundaji wa istilahi za Kiswahili za kwenye linux, kuna baadhi ya mbinu zilizotumika zinazoonyesha kuvunja kanuni na misingi ya uundaji istilahi. Kwa mfano kuna istilahi zilizoundwa kwa kukiuka msingi wa uundaji istilahi unaosema, istilahi sharti ziwe fupi na zenye kueleweka. Kuna baadhi ya istilahi ambazo ni ndefu na hivyo kukiuka huu msingi. Mfano:
·         Allow popup from this site    >    ruhusu udukizi kutoka tovuti hii
·         Com port      >        mlango wa mawasiliano
Istilahi hizi zimeonekana kuwa ndefu kwa sababu mbinu iliyotumika ni ya mwambatano wa maneno, na kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko wanasema, “iwapo istilahi zitaundwa kwa kutumia mbinu za muungano na mwambatano wa maneno basi mambo yafuatayo itabidi yazingatiwe”:
                  i.             Idadi ya maneno yanayounganishwa au yanayoambatanishwa yafaa yasizidi mawili.
                ii.            Vistari visitumike kutenga istilahi ambatani kwani katika Kiswahili istilahi za namna hii hutamkwa kama neno moja lenye mkazo mkuu kwenye silabi moja tu.
              iii.            Istilahi za namna hii yafaa zisiwe na silabi zaidi ya nane kwani kwa kawaida maneno ya Kiswahili yanawastani kati ya silabi moja na tano tu. Kwa msingi huu mifano ya itilahi zilizotolewa hapo juu zimeundwa na maneno zaidi ya mawili na silabi zaidi ya nane. Mfano ; mlango wa mawasiliano (silabi 10), ruhusu udukizi kutoka tovuti hii (silabi 15) na hivyo huu ni udhaifu uliojitokeza.
Vilevile matumizi ya mbinu za uhulutishi na upanuzi wa maana ya maneno yaliyopo zimetumika, huu ni udhaifu kwani misingi ya uundaji wa istilahi za Kiswahili inasema, mbinu ya

uhulutishaji iepukwe kwani etimolojia yake ina uvulivuli na uundaji wa istilahi kwa kupanua maana ya maneno yaliyopo yafaa uepukwe kwani istilahi za namna hii zinawakanganya wengi hasa zinapotumika nje ya muktadha au kwenye taaluma zenye mahusiano ya karibu.
Mifano ya istilahi zilizoundwa kwa uhulutishaji ni:
·         Taswidoti    >      bitmap
·         Medianuwai     >    multimedia
Na mfano wa istilahi iliyoundwa kwa upanuzi wa maana ya neno ni:
Puku    >    mouse. Puku ni istilahi iliyopanuliwa maana ambapo maana yake ya kawaida ni panya pori lakini maana yake maalumu ni kifaa kinachotumika katika utumiaji wa kompyuta.
Kwa hiyo huu ndio udhaifu wa istilahi zilizotumika katika uundaji wa istilahi za Kiswahili katika linux.

2.3.3 Mbinu bora zaidi katika uundaji wa istilahi za Kiswahili.
Kulingana na utafiti huu mbinu zilizoonekana kuwa bora zaidi na ambazo zinatumika sana katika uundaji wa istilahi za Kiswahili ni pamoja na, unyambulishaji, ukopaji, mwambatano, muunganiko pamoja na tafsiri mkopo. Mbinu hizi zimeonekana kuwa bora katika uundaji wa istilahi za Kiswahili kwa sababu zinaruhusu uundaji istilahi kwa wingi iwezekanavyo na mbinu hizi huzingatia misingi ya uundaji istilahi za Kiswahili. Misingi hiyo ni pamoja na ufaavu wa kiisimu, uwekevu wa kiisimu, unyambulifu , uwakilishi wa istilahi moja kwa dhana moja, udhahiri na utoshelevu pamoja na uangavu. Mbinu hizi huakisi kwa kiasi kikubwa misingi hii na hivyo kupendekezwa na waunda istilahi katika uundaji wa istilahi za Kiswahili.


                                            

                                             SURA YA NNE
   Muhtasri na Hitimisho
4.1 Matokeo ya utafiti kwa muhtasari
Utafiti huu umeongelea malengo matatu. Kwanza utafiti huu umebainisha mbinu za uundaji istilahi zilizotumika katika linux. Pili utafiti umepambanua ubora na udhaifu wa mbinu za uundaji istilahi za Kiswahili zilizotumika katika linux. Tatu umebainisha mbinu bora zaidi katika uundaji wa istilahi za Kiswahili.
Utafiti huu umeonyesha kuwa mbinu kumi za uundaji istilahi za Kiswahili zimetumika katika istilahi za linux. Mbinu hizo ni pamoja na:
Unyambulishi; mifano ya istilahi zilizoundwa kwa mbinu hii ni kama vile:
·         Ufikio   >    accessing
·         Utengaji   >   allocation
·         Alamisho   >    bookmark link
·         Ingizo   >    input
Muungano wa maneno; mifano ya istilahi zilizoundwa kwa mbinu hii ni pamoja na:
·         Ufichojina   >   anonymity
·         Mkwajunyuma   >   backslashes
·         Kanzidata     >      databank
Ukopaji; mbinu hii pia imetumika katika kuunda istilahi za kwenye linux. Mfano:
·         Akaunti    >   account
·         Apuleti      >   applet
·         Dayo      >      dial
Tafsiri mkopo (tafsiri sisisi); mifano ya istilahi zilizoundwa kwa kutumia mbinu hii ni:
·         Menyu vitendo    >    actions menu

·         Meneja ithibati    >    certificate manager
·         Paneli dhibiti     >       control panel
Mwambatano;  mbinu hii vilevile imebainishwa kutumika katka uundaji wa istilahi za Kiswahili  katika linux:
Mifano:   Rangi usuli    >     background color
                Orodha tobwe    >    bullet list
                Thamani upenyo   >    aperture value
Kuunda maneno mapya kabisa; mbinu hii pia imetumika. Mfano.
·         Ikoni    >   icon
·         Italiki    >    italic
·         Menyu proksi   >   menu proxies
Ufupishaji; katika utafiti huu mbinu hii pia imetumika. Mfano:
·         Kbdl (kibadala)   >   Alt (alternative)
·         Kdbt (kidhibiti)   >    Ctrl (control)
·         Epa (epuka)     >     Esc (escape)
·         KISARA (Kioneshi Sanifu Rasilimali )   >    URL (Uniform Resource Location)
Uhulutishi; mbinu hii pia imetumika. Mfano:
·         Taswidoti   >   bitmap
·         Medianuwai   >   multimedia
Upanuzi wa maana; mfano, puku (panya pori)   >   mouse.
Utemaji (clipping); mbinu hii pia imetumika. Mfano, kibonye   >   key (on keybody).
Kwahiyo hizi ndizo jumla ya mbinu zilizo tumika kuunda istilahi za Kiswahili katika linux.

Matokeo ya utafiti huu yanaonyesha mbinu zilizotumika ni bora kwa kiasi kikubwa hii ni kutokana na sababu kwamba, mbinu zilizotumika zimezingatia misingi na kanuni za uundaji istilahi kwa kiasi kikubwa. Lakini vilevile baadhi ya mbinu za uundaji istilahi zimetumika
 ambazo kwa mujibu wa misingi ya uundaji istilahi hazifai kutumiwa katika mchakato wa uundaji wa istilahi za Kiswahili. Mbinu hizi ni pamoja na uhulutishi na upanuzi wa maana ya maneno yaliyopo.
Pia utafiti huu umebainisha mbinu bora katika uundaji wa istilahi za Kiswahili kuwa ni unyambulishaji, muungano wa maneno, uambatishi, mkopo pamoja na tafsiri mkopo. Hii ni kwa sababu mbinu hizi huzingatia misingi ya uundaji wa istilahi za Kiswahili kwa kiwango kikubwa.

3.2 Hitimisho
Katika mchakato wa uundaji wa istilahi za Kiswahili kuna misingi ambayo hainabudi kufuatwa. Ili kuunda istilahi zilizobora mwanahistilahi hanabudi kuzingatia misingi hii.
Kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko (2008) wanasema kuwa ili kuinua ubora wa istilahi za Kiswahili waundaji istilahi wanasisitizwa kuzingatia mambo matatu muhimu. Kwanza wanasisitizwa kwa kadri iwezekanavyo wafuate kwa makini kanuni na taratibu za uundaji istilahi za Kiswahili. Kwa kufanya hivi itawezesha kwa kiwango kikubwa kuundwa istilahi za Kiswahili zenye kulandana vizuri kisarufi.
Pili waundaji istilahi wanahimizwa kuachana na mtindo wa kuunda istilahi moja moja kukidhi mahitaji yao ya istilahi ya papo kwa papo kwani mtindo huu unasababisha uundaji wa istilahi zisizo na mtiririko na  utimilifu wa kuridhisha. Kwa kuwa dhana zinazo wakilishwa na istilahi kwa kawaida huwa hazikai pweke pweke bali hukaa kama seti au mifumo maalumu, basi ni vema uundaji istilahi ufuate vilevile mifumo hiyo ya kidhana. Kulingana na maelezo haya kinachosisitizwa ni uundaji wa istilahi kwa kuzingatia mifumo ya kidhana. Kwa mujibu wa Tumbo-Masabo na Mwansoko (wameshatajwa) wakimnukuu Mkude (1989:34) wanasema,

uundaji wa istilahi kwa kuzingatia mfumo wa kidhana unafaida kuu nne:
(i)     Utawasaidia waunda istilahi kuonyesha wazi mantiki ya uhusiano baina ya istilahi za ukanda mmoja.
(ii)   Utawahimiza waunda istilahi kubainisha vizuri zaidi tofauti ndogondogo lakini muhimu baina ya istilahi zinazokaribiana.
(iii) Utawasaidia kutambua haraka mapengo katika nasaba au upungufu katika maelezo.
(iv) Utawasaidia waunda istilahi kuona haraka ni istilahi zipi zitaweza kuathiriwa upesi iwapo  kutatokea mabadiliko katika istilahi moja wapo.
Hivyo utaratibu wa uundaji istilahi kinasaba ukitumiwa utaepusha uundaji wa istilahi zinazogongana na zisizo na mtiririko wenye mantiki.
Jambo la tatu kama ilvyoainishwa na Tumbo-Masabo na Mwansoko ni kwamba uundaji wa istilahi haunabudi kuzingatia tofauti za watumiaji, mathalani viwango vyao vya elimu, mazingira yao na kadhalika. Kwa hali hii ili kuhakikisha istilahi bora za Kiswahili zinaundwa ni muhimu hadhira mahususi za watumiaji istilahi ziainishwe na istilahi ziundwe kufuatana na viwango vya elimu ya watumiaji lengwa. Ni kwa kufanya hivyo dhana kama vile istilahi angavu au istilahi zenye uvulivuli zitakuwa na maana halisi kwani zitahusishwa na vikundi mahususi vya watumiaji istilahi.

Na Aritamba Malagira.
Haki zote zimehifadhiwa. 








                                                 MAREJEO

Kahigi,K.K (2004).Ujanibishaji wa office na windows xp kwa Kiswahili sanifu katika
                 http//ajol.info.
Kiango,J.G (2004). Uundaji wa msamiti mpya katika Kiswahili: Zoezi lenye njia mbalimbali
                 katika Kiango.htm.
King’ei, K (2010). Misingi ya isimujamii. Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Msanjila,Y.P, Kihore,Y.M na D.P.B Massamba (2011). Isimujamii sekondari na vyuo.
                    Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Samson, H.R (1988). Ufundi wa magari, mfano wa ukuzaji wa istilahi za Kiswahili katika
                     Mulika na.21. Dar es salaam. Taasisi ya uchunguzi wa Kiswahili.
Sewangi,S.S (2004). Maana katika uundaji wa istilahi katika Sewangi,pdf.
Tumb-Masabo,Z.N.Z na Mwansoko,H.J.M (2008). Kiongozi cha uundaji istilahi za Kiswahili.
                       Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.



16 comments:

Anonymous said...

kazi nzuri sana shukrani

Unknown said...

Asante sana! Karibu Katika blogu hii, kama una kitu tunaweza kushirikiana.

Anonymous said...

Asante sana ndugu. Tafadhali nieleze kwa kifupi tu upungufu wa mbinu za ufupishaji wa maneno.

patience namukoli said...

sadakta mwana kaka

Unknown said...

Karibu sana!

Unknown said...

kazi nzuri sana, kwa hilo nakupa kongole

Unknown said...

Basi nisipotoa shukurani nitakuwa ni mkorofi wa aina gani? Kwa kweli sana maneno halisi ya kutumia kwa kuonyesha furaha yangu kwa utafiti huu hapa. Ahsante sana ndugu.

Redneka said...

Je, kuna tofauti kati ya unyambulishaji na uambishaji??

Nuru ya siha said...

Habari,
Nisaidie tafsiri ya neno BRAND

kolochatechee said...

hodi ni wewe katika haraka haja mkopo kulipia kuanza yako madeni ya kuanzisha biashara au nyumba ??? Kisha inakuja teksi kampuni una imani na relay juu ya 100% uhakika sababu hii ni kampuni ambapo i cashed mkopo wangu kwa mama yangu Stella dawa leo ili kuwasiliana na René Mikopo Firm halisi kupimwa na kuaminiwa na leo mimi nina furaha i got mkopo wangu wa $ 120,000 leo ili kupata kushikamana leo mrsstellareneloanfirm@hotmail.com} {barua pepe hapa chini na kupata jibu la matatizo yako yote kwa sababu Siwezi Kunyamaza ushuhuda huu mkubwa peke yangu binafsi ili i aliamua kuandika kwenye tovuti kwa sababu kula furaha kubwa kwa yangu moyo na leo mimi nina kuishi maisha mapya shukrani kwa wote Stella René


kolochatechee

Anonymous said...

Nakupa kongole kwa kazi nzuri. Katika utafiti wako nimeona maneno haya yamechangaywa kidogo, Je Mause ni punu au crop ndio punu? Kuna mahala umeita mouse=Punu na kuna mahala umeita Crop=Punu. Ufafanuzi please.

Unknown said...

Habari ndugu,

Nadhani hukuangalia vizuri maneno hayo "Mouse" na "Crop" tofauti zake zimewekwa bayana. "Mouse" ni "Puku" na "Crop" ni "Puna".

Unknown said...
This comment has been removed by the author.
Unknown said...
This comment has been removed by the author.
GLORY BENSON said...

Niko hapa kutoa ushuhuda kubwa Nimejaribu michache ya jukwaa wengine wote katika kutafuta nzuri kampuni mkopo ambayo itasaidia yangu kwa mkopo kwa bahati mbaya kwa ajili yangu mimi kukutana 3 mkopo kampuni waliokuwa tu baada ya kile mimi naweza kuwapa na si kusaidia me walichukua fedha kutoka kwangu na hamkunipa majibu yoyote chanya wote I got ilikuwa hadithi. Kisha mimi nikajikuta uchapishaji kutokana na huduma mkopo na tu aliamua Email na kusikia kile got kusema lakini basi mimi aligundua kwamba wao alizungumza vizuri na akapiga halisi mimi kufundishwa kuhusu hilo na akawapa kesi hiyo. Hatimaye I got mkopo masaa 24 tu baada ya mazungumzo kama kwamba alikuwa si wote mimi got kukutana mkopo katika akaunti yangu jioni ya pili ya siku mimi aliwasiliana nao. wow! hatimaye kitu kimoja kwamba Ilinichukua miaka ya kupata kutoka kampuni nyingine mkopo pia mimi masaa 24 tu kupata kutoka kwao. Tangu wakati huo mimi tumeamua kusaidia Msemaje na kutangaza yao kwa watu ambao kukutana kuwa katika viatu nilikuwa au kwa watu ambao wanahitaji huduma hapa ni pale kampuni pepe: diamondloancompany01@yahoo.com kuwapa kesi na kumshukuru mimi baadaye hawana hata kujua nafanya hivyo. njia tu kidogo ya kusema Asante.

Justine majaliwa said...

kazi nzuri