Friday, March 16, 2012

KISWAHILI NA UKALIMANI

Dunia inabadilika kila kukicha, sayansi na teknolojia huibuliwa kila kukicha, mambo haya yote huwaweka watu pamoja kutoka kila kona ya dunia, lakini pia watu hawa hawzungumzi lugha moja, wanahitaji kuwasiliana na ili mawasiliano yaweze kufanyika lazima kuwepo na lugha inayowaunganisha. Suala hili ni gumu kwa kuna lugha nyingi sana duniani na kila nchi inasera yake juu ya lugha lakini pia lazma watu wawasiliane na hapa ndipo tunaona umuhimu wa kuwepo mkalimani. 
Lugha ya kiswahili inakuwa kwa kasi sana, vyuo mbalimbali duniani hufundisha lugha hii adhimu kwa nini wewe usione fursa hii na uchukue hatua ya kujifunza ukalimmani ili ujiajiri katika soko kubwa kama hikli.
Kabla hujachukua uamuzi hebu jielimishe kidogo juu ya taaluma hii ya ukalimani.


Tafsri na ukalimani ni taaluma za lugha ambazo mara nyingi watu huchanganya wakidhani kuwa dhana hizi mbili hufanana lakini kimsingi kuna utofauti mkubwa kati ya tafsiri na ukalimani, elimu na ujuzi katka taaluma hizi hutofautiana. Kuna tofauti za msingi zinazotofautisha taaluma hizi, tutazichambua kwa kina katika sura zinazofuata. Kwa sasa tuangalie kwa kina dhana nzima ya ukalimani ambapo tutaangalia maana, aina za ukalimani, sifa za mkalimani (mambo ya kuzingatia katika ukalimani) na mwisho hitimisho.
Maana ya ukalimani.
Ukalimani wa lugha hulenga kurahisisha mawasiliano ya lugha ya mdomo au lugha ya alama kati ya watumiaji wa lugha mbili tofauti.
Kwa mujibu wa Encarta (2009) ukalimani ni tafsiri ya mdomo ya kile kinachosemwa katika lugha moja kwenda lugha nyingine ili kusudi wazungumzaji wa lugha tofauti waweze kuwasiliana.
Wikipedia wamefasili ukalimani kuwa ni uhawilishaji wa ujumbe katika lugha ya mazungumzo au lugha ya alama kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine.
Fasili zote hizi zinajaribu kutupa mwangaza hasa juu ya maana ya ukalimani, fasili ya kwanza inakasoro. Kutumia istilahi yenye maana tofauti na kile kinachojaribu kufasiliwa huleta mkanganyiko, istilahi tafsiri inamaana tofauti na ukalimani kwa hiyo sio sahihi kuitumia katika kufasili dhana ya ukalimani. Fasili ya pilli imejaribu kugusa mambo muhimu katika dhana ya ukalimani, kwamba ni uhawilishaji wa ujumbe katika lugha ya mazungumzo, kimsingi ukalimani hufanyika katika lugha ya mazungumzo.
Kwa hiyo kutokana na fasili hizi tunaweza kupata fasili ya jumla kwamba, ukalimani ni zoezi la uhawilishaji wa mawazo,ujumbe, maana katika lugha ya mazungumzo au lugha ya alama kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa.
Hivyo basi mkalimani ni mtu ambaye huhawilisha mawazo, maana au maelezo kutoka lugha chanzi na kuyaweka mawazo au maelezo au maana yenye maana inayolingana katika lugha lengwa, katika wakati halisi. Kazi ya mkalimani ni kufikisha kila kipengele cha kisemantiki (rejesta,toni) na kila lengo na hisia za ujumbe ambao mzungumzaji wa lugha chanzi amekusudia kufikisha katika wapokeaji wa lugha lengwa.
Aina za ukalimani.
Kuna aina tofautitofauti za ukalimani kulingana na vigezo tofautitofati vinavyotumika katika kuainisha aina za ukalimani. Kwa kutumia kigezo cha jinsi ukalimani unavyofanywa, tunapata aina kuu mbili:
Ukalimani mfululizo; katika ukalimani wa aina hii mzungumzaji wa lugha chanzi na mzungumzaji wa lugha lengwa huanza pamoja na kumaliza pamoja. Maranyingi vifaa maalum hutumika, mkalimani hukaa katika chumba chenye kidhibiti sauti akizungumza kupitia kipaza sauti wakati huo akimsikia na kumwona barabara mzungumzaji wa lugha chanzi kupitia visikizio. Wasikilizaji wa lugha lengwa hupata ujumbe kupitia visikizio. Vilevile ukalimani wa aina hii hutumiwa sana na wakalimani wa lugha ya alama.
Ukalimani fuatizi; katika aina hii ya ukalimani, mkalimani huzungumza baada ya mzungumzaji wa lugha chanzi kumaliza kuzungumza. Mkalimani anakua amesimama au amekaa sambamba na mzungumzaji wa lugha chanzi akiwa anasikiliza napengine kuandika maneno anayozungumza mzunguzaji wa lugha chanzi ili kumsaidia kukumbua pindi atakapoanza kukalimani. Wakati mzingumzaji wa lugha chanzi anapumzika au anamaliza kuongea ndiposa mkalimani anahawilisha kipande cha ujumbe au ujumbe mzima katika lugha lengwa.

Aina zingine za ukalimani.
Ukalimani wa kwenye mikutano; huu ni ukalimani unaofanyika wakati wa mikutano, huweza ukawa fuatizi au mfululizo, lakini kwa sababu ya mikutano inayokutanisha lugha nyingi, ukalimani fuatizi hautumiki. Katika ukalimani wa kwenye mikutano maranyingi mkalimani hufanya ukalimani kutoka lugha za kigeni kwenda lugha yake ya asili.
Ukalimani wa mahakamani; ukalimani wa aina hii hufanyika mahakamani, katika mabaraza ya kutolea hukumu na mahali popote pale ambapo masuala ya kisheria hufanyika, mfano katika kituo cha polisi hususani wakati wa kuchukua maelezo au katika ukumbi wa mikutano kwa ajili ya kuapishwa.
Ukalimani kiungo; ukalimani wa aina hii ni pale ambapo mkalimani humsaidia mtu au kikundi cha watu katika kutalii, matembezi au katika mkutano.
Ukalimani wa lugha ya alama; hii ni aina ya ukalimani ambao hufanyika kati ya lugha ya alama na lugha ya mazungumzo. Mzungumzaji anaweza kuongea mkalimani akahawilisha mawazo kwa njia ya alama, vilevile wakati mtu asiyesikia akifanya mawasiliano kwa lugha ya alama, mkalimani atahawilisha maana katika lugha ya mazungumzo. Vilevile ukalimani huweza kufanyika kati ya lugha ya alama na alama hii ni kwa sababu lugha ya alama hutofautiana kati ya nchi na nchi.
Ukalimani wa vyombo vya habari; kulingana na asili yake ukalimani wa vyombo vya habari hufanyika kwa ukalimani mfululizo. Hufanyika zaidi katika matangazo ya moja kwa moja ya televisheni au redio. Katika ukalimani wa vyombo vya habari vifaa kama  chumba cha kudhibiti sauti, kiwamba nakadhalika huhitajika sana.
Ukalimani wa simu; ukalimani wa aina hii humsaidia mkalimani kufanya ukalimani kupitia simu. Maranyingi hufanyika katika mazingira ambayo watu wanaohitaji kuwasiliana tayari wanakuwa wamekwishazungumza kupitia simu.
Ukalimani wa video; ukalimania wa aina hii hufanyika katika mazingira ambapo mmoja kati ya wanaowasiliana ni kiziwi au hasikii vizuri au hawezi kuongea (bubu). Katika mazingira kama haya ukalimani wa lugha ya alama hufanyika zaidi.
Ukalimani kulingana na muktadha; katika kundi hili kuna aina nyingi kulingana na jinsi itakavyojidhihirisha aktika miktadha tofautitofauti. Mfano, ukalimani wa kanisani, ukalimani wa msikitini, ukalimani wa mahakamani, jeshini nakadhalilka.
Ni matumaini ya ngu utakuwa umenufaika, unaweza pia kutoa maoni yako!.

20 comments:

Anonymous said...

tofauti iko wapi kati ya ukalimani na utafsiri?

Unknown said...

Asante sana kwa swali lako zuri. Karibu katika blogu hii!

Kwa kweli watu wengi wanadhani kuwa tafsiri ni sawa na ukalimani, hii sio sahihi. Ukalimani na tafsiri ni taaluma za lugha ambazo zina uhusiano wa karibu lakini pia kwa nadra sana watu wachache huweza kuzimudu vizuri taaluma zote hizi kwa kiwango kilekile. Tofauti katika ustadi, mafunzo, kipaji na hata uelewa mzuri wa lugha ni mambo muhimu sana katika taaluma za tafsiri na ukalimani ambayo watu wachache wanaweza kufanikiwa kuwa nayo kwa kiwango cha taaluma. Kwa hiyo kwa misingi hiyo, kunatofauti kati ya taaluma ya tafsri na ukalimani, tofauti hizo ni kama hizi rafiki:

i) Tafsiri hufanyika kwa njia ya maandishi, mfasiri huhawilisha mawazo au ujumbe kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa kwa kutumia kalamu na karatasi au kwa kuchapa kwa kutumia kompyuta kinyume na ukalimani, mkalimani huhawilisha kile anachosema mzungumzaji wa lugha chanzi kwenda lugha lengwa kwa njia ya mdomo.

ii) Tafsiri hufanyika kwa kurejelea marejeo mbalimbali kama vile kamusi za aina zote zinazohusika na matini husika pamoja na marejeo mengine muhimu ilihali ukalimani hufanyika bila kurejelea mahali popote.

iii) Katika tafsiri, mfasiri ni lazima asome kwanza matini chanzi kabla haajanza kufasiri kwa lengo la kuihakiki ili aweze kutoa zao bora zaidi la tafsiri lakini katika ukalimani si lazima mkalimani apitie matini chanzi kabla ya kuanza kukalimani kwani ukalimani hufanyika hapo kwa papo.

iv) Katika tafsiri mfasiri ana muda wa kuihakiki matini anayoifasiri ili aweze kurekebisha makosa yanayojitokeza kabla ya kuikabidhi kwa mteja lakini katika ukalimani, mkalimani hana muda wa kufanya marekebisho.

v) Mafunzo yanayotolewa kwa mfasiri ni tofauti na yanayotolewa kwa mkalimani. Mfasiri hufundishwa stadi za uandishi na usomaji mzuri ilihali mkalimani hufundishwa stadi za kuzungumza vizuri mbele ya umma.

vi) Katika ukalimani, mkalimani ni lazima awe na uelewa wa kiwango sawa katika lugha zote mbili yaani lugha chanzi na lugha lengwa, hii ni kwa sababu mkalimani anaweza kulazimika kukalimani kwenda pande zote mbili kwa wakati huohuo lakini kwa mfasiri sio lazima sana aielewe lugha chanzi kwa kiwango sawa na cha luhga lengwa.

vii) Ukalimani hufanyika katika muda halisi yaani zao la ukalimani ni la hapo kwa papo wakati tafsiri haifanyiki katika muda halisi mfasiri anaweza kufanya kazi yake muda wowote kulingana na uhitaji wa mteja wake.

Natumaini utakuwa umeiona tofauti. Karibu sana tushirikiane katika taaluma hii ya Kiswahili.

Unknown said...

samahani me hapa nimeelewa lakini swali langu linakuja kuwa taaluma ya kutafsiri inamwingiliano na kazi nyingine za kiswahili, je zinaingiliana vipi? na hizo kazi ni zipi?

Unknown said...

Asante kwa swali lako zuri ndungu! Ila sina uhakika kwamba unaposema kazi nyingine za kiswahili unamaanisha nini. Lakini kulingana na swali lako naweza nikakujibu hivi; Taaluma ya Kiswahili haipo peke yake ina mwingiliano mkubwa na taaluma nyingine, kama swali lako kweli lipo kwenye kazi nyingine za kiswahili naomba ufafanue kidogo ili uliweke wazi swali lako.

Lakini kwa kuanza nitalijubu swali lako kama ifuatavyo, kama utaridhika naomba unijulishe. Kama nilivyosema kuna mwingiliano mkubwa kati ya tafsiri na taaluma nyingine na taaluna hizo ni hizi zifuatazo:

Taaluma za kiisimu

Semantiki; hii inahusiana na maana. Katika tafsiri tunazingatia maana ya lugha chanzi ili isitofautiane na maana ya lugha lengwa. Muktadha pia sharti uzingatiwe katika kupata maana.

Isimujamii; huangalia jamii inavyoathiri lugha na lugha inavyoathiri jamii. Katika tafsiri tamaduni, mila na desturi za jamii husika huzingatiwa. Mfano unapokutana na maneno ya kitamaduni katika tafsiri kv salamu, vyakula n.k hapa inabidi utamaduni wa lugha husika uzingatiwe.

Isimu linganishi; katika tafsiri tunalinganisha lugha moja na nyingine ili kuelewa miundo na maumbo kati ya lugha chanzi na lugha lengwa, kwa hiyo isimu linganishi huchukua nafasi yake hapa.

Elimu mitindo; katika tafsiri kuna uainishaji wa mitindo ya lugha na muktadha wa matumizi yake kitu ambacho kipo katika taaluma ya elimu mitindo.

Taaluma zisizo za kiisimu

Uhakiki wa matini; katika tafsri kabla mfasiri hajaanza kutafsiri matini ni lazima ahakiki matini chanzi kwa lengo la kubaini upungufu unaojitokeza na ili kujua namna ya kuweza kukabiliana nao.

Mantiki; hii ni taaluma inayohusu ukweli na usahihi katika kauli au matini Fulani. Taaluma hii humsaidia mfasiri kubaini mfasiri kubaini usahihi na mantiki iliyopo katika lugha chanzi

Falsafa; hii ni taaluma inayosisitiza kutafuta maana za maneno kutokana na matumizi halisi katika matini. Hii humsaidia mfasiri kujua falsafa ya matini husika ili kujua maana yake.

Hata kama nitakuwa sijalijibu swali lako lakini nadhani nitwakuwa nimekupa mwanga fulani na nafikiri unaweza kuliweka sawa swali lako vizuri.

Anonymous said...

uja tupa umuhimu wa ukalimani na tafsiri kwenye ulimwengu wa sasa

Unknown said...

nashukulu kwa kunijibia swali langu lkn swali lenyewe liko hivi, taaluma ya kutafsiri inafanya kazi kwa ujirani au mwingiliano na taaluma nyingine ambazo ni za lugha, taja angalau taaluma tano zinazofanya kazi kwa kushirikiana na taaluma hiyo alafu elezea kwa mifano ni kwa vipi zinaingiliana na taaruma ya kazi ya tafsiri. namba msaada

Unknown said...

Sawa, nafikiri hilo swali ndilo nimelijibu, jibu lake ndo hilo nililokwishalijibu. Taaluma nyingine za lugha ndo kama hizo, uhakiki, isimu linganishi, isimujamii, elimu mitindo na nynginezo kama hizo. Jibu lako likijikita hapo utakuwa umejibu swali lako vizuri.

Unknown said...

Asante kwa kazi nzuri, naomba unisaidie vigezo vya uainishaji wa ukalimani

Unknown said...

Vizuri sana mtaalamu naomba unisaidie dhana kama nne tofauti za ukalimani

Kitambulio said...

Ningependa kujuzwa Umuhimu wa tafsiri na ukalimani katika mawasiliano

Khamicinho Mkocevic said...

Ukipewa nafasi ya kukutana na wajumbe wa katiba 2014 wa bunge la jamuhuri ya Tanzania utawashawishi vipi kuhusu ukalimani

Mlelwa04 said...

Naomba kujua aina za ukalimani kwa kutuMia kigezo cha lugha na muktadha

Unknown said...

Kazi nzuri Sana kaka,lakini wanataaluma wengi Sana dhana ya ukalimani inawakanganya hasa kwakua wanaona ukalimani na tafsiri ni dhana moja. Je wewe Kama mwana taaluma una mtazamo gani kuhusu ilo?

Unknown said...

Asante kwa Nazi nzuri

Unknown said...

Asante kwa Nazi nzuri

Unknown said...

Swali langu ni naomba unitajie mifanano iliyopo kati ya ukaliman n tafsiri

Unknown said...

Mkalimani ni kipaza sauti cha mzungumzaji wa lugha chanzi ingawa sio kwa kila jambo. Jadili kwa hoja ukweli na usikweli wa madai haya. Naomba msaada wa majibu

Unknown said...

Swali langu ni eleza wahusika katika ukalimani

Anonymous said...

Mambo ya msingi unapofasili lugha

Anonymous said...

tofauti kati ya ukalimani wa kutumiya lugha ya maneno n ukalimani wa kutumiya lugha ya alama