Isimu



    HISTORIA YA KISWAHILI

Kwa kuwa msamiati mwingi uliopo katika lugha ya Kiswahili unatokana na lugha ya kiarabu ni dhahiri kuwa lugha hii inatokana na kiarabu. Jadili.


 Katika kujadili swali hili tutaanza na utangulizi kwa kueleza  maana ya asili, maana ya msamiati na baada ya hapo tutaangalia jinsi kigezo cha msamiati kinavyotumiwa kudai kuwa Kiswahili ni kiarabu na tutaonesha udhaifu wake na mwisho tutakanusha madai haya kwa kuonesha kuwa Kiswahili ni kibantu na sio kiarabu.
Mjadala kuhusu asili ya Kiswahili umejadiliwa na wataalam mbalimbali na wametumia vigezo mbalimbali kuthibitisha madai yao. Wapo wanaodai kuwa Kiswahili ni kiarabu, wanaoshadidia dai hili, kigezo kimojawapo wanchokitumia ni kigezo cha msamiati, kwamba lugha ya Kiswahili ina msamiati mwingi wa kiarabu na kwa hiyo kwakuwa Kiswahili kina msamiati mwingi wa kiarabu basi pia Kiswahili ni kiarabu, kwa kweli dai hili halina mashiko. Kabla hatujaanza kufafanua kwamba kwa nini dai hili halina mashiko  ni vema tukaangalia fasili ya dhana muhimu kama zinavyojitokeza katika swali la mjadala. Dhana hizo ni kama zifuatazo:
‘Istilahi asili,’ kwa mujibu wa Massamba na wenzake (1999:3) asili ni jinsi  kitu au jambo lilivyotokea au lilivyoanza.  Fasili hii ni nzuri na inajitosheleza kwa maana kwamba jambo au kitu kinaweza kutokea kibahati kama ilivyo katika lugha au linaweza kuanzishwa.
Msamiati kwa mujibu wa TUKI (2004) ni jumla ya maneno katika lugha. Fasili hii iko wazi kwamba jumla ya maneno yote katika lugha ndio huunda msamiati wa lugha husika.
Wataalam wanaodai kuwa Kiswahili ni kiarabu kwa kutumia kigezo cha msamiati, hoja zao ni kama zifuatazo:
Khalid (2005) anasema kuwa neno lenyewe Kiswahili limetokana na neno la kiarabu sahil katika umoja ambalo wingi wake  ni sawahili likiwa na maana ya pwani au upwa. Hivyo kutoka na  jina la lugha hii ya Kiswahili kuwa na asili ya neno la kiarabu sahil hivyo hudai kuwa Kiswahili ni kiarabu.
Khalid anaendelea kusema kuwa Kiswahili kina msamiati mwingi wenye asili ya kiarabu. Hapa ni baadhi ya mifano ya msamiati wa Kiswahili wenye asili ya kiarabu kama alivyobainisha Khalid:
Maneno yanayoonesha muda.
Asubuhi                         dakika 
Wakati                            alfajiri
Karne                              alasiri
Magharibi                       saa
Maneno yanayowakilisha namba.
Nusu                             robo
Sita                               saba
Tisa                              ishirini
Thelathini                     arubaini        
Hamsini                        sitini
Sabini                           themanini
Tisini                             mia
Elfu
Mtandao wa jamiiforum pia wameonesha  mifano ya msamiati wa Kiswahili wenye asili ya kiarabu kama ifuatavyo:
Kiswahili                            Kiarabu
Dirisha                                drisha
Karatasi                              kartasi
Debe                                   dabba
Samaki                                samak
Mustakabali                        mustakabal
Madrasa                               madrasa
Lodh (2000:97) naye anasema kiasi kikubwa cha nomino za Kiswahili zimetokana na mizizi ya maneno ya kiarabu. Mifano ya maneno hayo ni kama yafuatayo:
Hesabu/hisabu     mahisabu/hisabati
Harka                   harakati
Safiri        -           msafiri
Safari   -               msafara
Fikiri    -              fikara/fikra
Hata hivyo kigezo hiki cha msamiati kina udhaifu; Massamba (2002) ameonesha udhaifu wa kigezo hiki kuwa ni pamoja na kwamba:
Hakuna ushahidi wowote wa kitakwimu ambao unaonesha idadi ya maneno ya kiarabu  yaliyopo katika lugha ya Kiswahili yanayoweza kuhitimisha kuwa Kiswahili ni kiarabu.
Kigezo cha msamiati peke yake hakijitoshelezi kuelezea kuwa Kiswahili ni kiarabu, walipaswa waangalie vigezo vingine kama vile kigezo cha kihistoria kwa kuchunguza masimulizi mbalimbali ya kale na kigezo cha kiisimu; katika kigezo hiki walipaswa kuchunguza fonolojia, mofolojia , na sintaksia ya Kiswahili kwa kulinganisha na kiarabu na ndipo wangepata hitimisho sahihi la madai yao.
Vilevile kigezo hiki cha msamiati hakina mashiko kwa sababu lugha ina tabia ya kuathiriana, lugha huathiriana na lugha nyingine endapo kutakuwa na mwingiliano baina ya wanajamii lugha hizo.  Kwa mfano Kiswahili kimetokea kuathiriana na kiarabu kutokana na uhusiano uliokuwepo hapo zamani katika biashara kati ya waarabu na watu wa upwa wa Afrika Mashariki na hii ikapelekea msamiatia wa kiarabu kuingia katika lugha ya Kiswahili, hivyo kwa hoja hii hatuwezi kusema Kiswahili ni kiarabu kwa sababu msamiati wa kiarabu unaonekana katika lugha ya Kiswahili.
Hata hivyo si lugha ya kiarabu tu ambayo msamiati wake unaonekana katika lugha ya Kiswahili vilevile kunamsamiati wa lugha zingine za kigeni katika lugha ya Kiswahili kwa mfano, neno lenye asili ya kireno katika Kiswahili ni kama vile meza, leso pia yapo maneno yenye asili ya kijerumani kwa mfano schule kwa Kiswahili shule na maneno yenye asli ya kiingereza ni kama vile mashine, televisheni, sekondari, redio, kompyuta na maneno mengine yenye asli hiyo. Basi ingekuwa msamiati wa kigeni kuonekane kwenye lugha fulani huifanya hiyo lugha kuwa na asili ya lugha ya kigeni basi tungesema pia Kiswahili ni kiingereza  kwa sababu tu msamiati mwingi wa kiingereza unonekana katika Kiswahili.
Pia kigezo hiki kinaonekana kuwa ni dhaifu kwa sababu hawakufanya utafiti katika nyanja zote za matumizi ya lugha kwa mfano msamiti unaotumika katika nyanja ya elimu, afya, utamaduni na kadhalika. Kwa hiyo madai haya yanaonekana kutokuwa na mashiko kwa ufinyu wa utafiti wake.
Kutoka na kigezo hiki cha msamiati kutokuwa na mashiko kuhitimisha kuwa Kiswahili ni kiarabu, basi hatuna budi kusema kuwa Kiswahili sio kiarabu bali ni kibantu. Katika kuthibitisha madai haya tutajikita zaidi katika kigezo cha kiisimu ambacho tunaamini kuwa ni kigezo pekee kinachoweza kutupatia taarifa sahihi kwani ni kigezo cha kisayansi lakini pia tutaangalia kwa ufupi vigezo ambavyo vinatoa ushahidi juu ya ubantu wa Kiswahili ambavyo ni ushahidi wa kihistoria, kiakiolojia na kiethinolojia. 
Kigezo hiki cha kiisimu kimetumiwa na wataalam mbalimbali katika kuonesha ubantu wa Kiswahili Massamba (ameshatajwa) amewataja wataalam mbalimbali ambao wamehusika na utafiti juu ya ubantu wa Kiswahili, wataalam hao ni pamoja na Carl Meinhof katika kitabu chake cha Introduction to the phonology of the Bantu language,  Duke (1935 – 1945), Malcom Guthrie (1967), Dereck Nurse na Thomas Spear (1985). Hawa walijadili ubantu wa Kiswahili kwa kutumia kigezo cha kiisimu, kihistoria na kiakiolojia.
Kwa kuanza na  kigezo cha kiisimu tutaangalia vipengele kama vile kufanana kwa msamiati wa msingi, muundo wa kifonolojia, muundo wa kimofolojia, muundo wa kisintaksia mpangilio wa ngeli za majina.
Mizizi ya msamiati wa msingi wa lugha za kibantu na Kiswahili hufanana kwa kiasi kikubwa, mifano ifuatayo huweza kuonesha ukweli huu.
Mfano,
Kiswahili
Kikurya
Kinyiha
Kijita
Maji
Amanche
Aminzi
Amanji
Jicho
Iriso
Iryinso
Eliso                              
Katika mifano hiyo hapo juu tunaona mifano hiyo hapo juu tunaona kuwa mizizi maji, manche, minzi, manji inafanana kwa kiasi kikubwa, kwa hiyo huu ni ushahidi tosha kutuonesha kuwa kuna uhusiano wa kinasaba kati ya Kiswahili na lugha za kibantu.
Pia mofolojia ya Kiswahili na lugha za kibantu hufanana kwa kiasi kikubwa, yaani mfumo wa maumbo ya maneno ya lugha ya Kiswahili na lugha za kibatu hufanana. Kwa mfano, namna viambishi vinavyopachikwa katika mzizi wa maneno hufuata kanuni ileile kama inavyotumika katika lugha ya Kiswahili yaani viambishi vinaweza kupachikwa kabla au baada ya mzizi na uwa na uamilifu bayana. Hebu tuchunguze mifano ifuatayo:
Kiswahili
Kisukuma
Kisimbiti
Kinyiha
A-na-lim-a
a-le-lem-a
a-ra-rem-a
i-nku-lim-a
a-na-chek-a
A-le-sek-a
a-ra-sek-a
a-ku-sek-a                               
  Kwa kuangalia mifano hii utagundua kwamba katika kutenganisha viambishi hufuata kanuni moja kwamba mahali kinapokaa kiambishi kwa mfano cha njeo, ndipo pia hukaa kwa upande wa lugha za kibantu, kwa mfano –na- na –ra- katika lugha ya kisimbiti. Hivyo tunaweza kusema kuwa kuna unasaba baina ya lugha hizi.
Vilevile sintaksia ya lugha ya Kiswahili na lugha za kibantu hufanana kwa karibu sana. Kwa mfano jinsi ya mpangilio wa vipashio na kuunda sentensi hufanana yaani mpangilio wa maneno hufuata kanuni maalum ambazo hufanana katika Kiswahili na lugha za kibantu. Katika Kiswahili sentesi ina kuwa na pande mbili yaani upande wa kiima na upande wa kiarifu, katika upande wa kiima kipashio chake kikuu ni nomino na katika upande wa kiarifu kipashio chake kikuu ni kietnzi. Hii inamaana kwamba katika kuunda sentensi ni lazima nomino ianze na baadaye kitenzi. Hebu tuangalie mifano ifuatayo:



Kiswahili
Mama / anakula
N (K)           T (A)
Kijita
Mai /   kalya
N(K)  T (A)      
Kihehe
Mama/ ilya
N(K)  T(A)
Kihaya
Mama / nalya
N(K)     T(A)
  Katika mifano hii tumeona kwamba muunndo wa kiima-kiarifu katika lugha za kibantu unafanana sana na ule wa Kiswahili yaani nomino hukaa upande wwa kiima halikadhalika kitenzi hukaa upande wa kiarifu, kwa hiyo kwa mifano hii tunaweza kusema kuwa lugha ya Kiswahili ni jamii ya lugha za kibantu.
Pia mfumo wa sauti (fonolojia) wa lugha za kibantu unafana sana na ule wa Kiswahili, yaani mpangilio wa sauti katika kuunda silabi, na miundo ya silabi kwa ujumla hufanana. Kwa mfano katika lugha ya Kiswahili hakuna muundo wa silabi funge yaani silabi ambayo inaishia na konsonanti, muundo asilia wa silabi za Kiswahili ni ule unaoishia na irabu vilevile katika lugha za kibantu hufuata muundo wa silabi wazi, yaani silabi zote huishia na irabu. Mifano ifuatayo hufafanua zaidi:
Kisawhili
Baba
K+I+K+I
Kikurya
Tata
K+I+K+I
Kiha
Data
K+I+K+I
Kijita
Rata
K+I+K+I
Kipare
Vava
K+I+K+I
Tanbihi: K= konsonanti I= irabu.
Kwa mifano hii tunaona kwamba mifumo ya sauti katika lugha za kibantu hufanana na ule wa Kiswahili, kwa hiyo tunaweza kuhitimisha kwa kusema kuwa lugha hizi ni za familia moja.
Pia vilevile mfumo wa ngeli za majina katika lugha ya Kiswahili hufanana sana na ule wa kibantu hususani katika upachikaji wa maumbo ya umoja na wingi na maumbo ya upatanisho wa kisarufi. Katika lugha ya Kiswahili viambishi vya umoja na wingi hupachikwa mwanzoni kabla ya mzizi wa neno, hivyohivyo katika lugha za kibantu. Kwa mfano:

Umoja
Wingi
Kiswahili
m-tu
wa-tu
Kikurya
mo-nto
abha-nto
Kiha
umu-ntu
abha-ntu
Kikwaya
mu-nu
abha-nu
Mifano hiyo hapo juu inadhihirisha wazi kwamba vipashio vyote vya umoja na wingi hujitokeza kabla ya mzizi wa neno, hivyo ni dhahiri lugha hizi zina uhusiano wa nasaba moja.
Vilevile katika upatanisho wa kisarufi lugha  za kibantu na Kiswahili huelekea kufanana viambishi vya upatanisho wa kisarufi hususani viambisha vya nafsi.
Kwa mfano:
Kiswahili
Mtoto a-nalia
Kizanaki
Umwana a-rarira
Kisukuma
Ng’wana a-lelela
Kikurya
Omona  a-rakura
Tunaona hapo juu kwamba kiambishi ‘a’ cha upatanisho wa kisarufi hujitokeza katika lugha zote, hivyo tunashawishika kusema kuwa Kiswahili kina uhusiano mkubwa  na kibantu.
Pamoja na ushahidi wa kiisimu kutupatia vithibitisho tosha juu ya ubantu wa Kiswahili pia kuna ushahidi mwingine kama vile ushahidi wa kihistoria, kiakiolojia na kiethinolojia.

Ushahidi wa kihistoria huchunguza masimulizi na vitabu mbalimbali vya kale ambavyo huelezea asili na chimbuko la wakazi wa upwa wa Afrika Mashariki. Vilevile ugunduzi wa  kiakiolojia huonesha kuwa kulikuwa na wakazi wa asili wa upwa wa Afrika Mashariki ambao walikuwa na utamaduni wao na maendeleo yao hata kabla ya kuja kwa wageni. Katika ushahidi wa kiethinolojia, huchunguzwa tarihi mbalimbali zinazojaribu kutoa historia ya watu pwani ya Afrika Mashariki na lugha yao.
Kwa ujumla vyanzo hivi vyote huonesha kuwa pwani ya Afrika mashariki ilikuwa na wakazi wake wa asili ambao walikuwa na lugha yao, utamaduni wao na pia maendeleo yao, vyanzo hivi pia huhitimisha kwa kusema kuwa lugha ya wakazi hawa ilikuwa ni Kiswahili.

Kwa hiyo, kwa hoja hizi tunaweza kuhitimisha kwa kusema kuwa, madai ya kusema kwamba msamiati mwingi wa kiarabu  katika lugha ya Kiswahili hayana mashiko; Kwani hakuna ushahidi wa kutosha kusimamia hoja hiyo. Kama ilvyojadiliwa hapo juu, vigezo vya kiisimu, kihistoria, kiakiolojia na kiethnolojia ndivyo vitoavyo ushahidi wa kina na kutoa hoja zenye mashiko kuthibitisha kuwa Kiswahili  sio kiarabu na badala yake Kiswahili ni kibantu.      

Insha hii imeandaliwa na wanafunzi wa Kiswahili Chuo Kikuu Cha Dar es salaam kama kazi ya kuwasilisha darasani,

23 comments:

Anonymous said...

kazi nzuri sana. mapendekezo yangu ni kuwa kazi hii ingepakiwa tena baada ya kusahihishwa na mwalimu wa somo ili kama ku mapungufu tuweze kutambua ili na sisi tusiyarejelee makosa hayo

Unknown said...

Usiwe na wasiwasi, kazi hii imesahihishwa, na mapendekezo ya mwalimu yammejumuishwa hapa, unaweza ukarejelea tu.

Anonymous said...

Safi sana kwa kazi yenu nzuri.

Anonymous said...

sadakta,maendelezo mazuri,ombi langu ni insha hii ihifadhiwe kwa manufaa ya kizazi kilichoko na kijacho.

Anonymous said...

kazi nzuri sana.DANIEL NALINGIWA from JOKUCO

Unknown said...

Asante! Karibu katika Blogu hii!

Anonymous said...

Azima unayo,uwezo unao, ujuzi unao himiza zaidi na ustadhi utauwahi. Hongera!

Unknown said...

Asante sana! Karibu sana katika neno thabiti.

Anonymous said...

uhusiano wa fonolojia na mofolojia

Unknown said...

Kazi mufti na yenye manufaa kwa yeyote afanyaye kozi kuhusu chimbuko la kiswahili
MWANAFUNZI KUTOKA CHUO KIKUU CHA NAIROBI

Unknown said...

Karibu ndugu Alio!

Anonymous said...

Hongera kwa kazi nzuri ya kusaidia wakereketwa wa lugha tukufu ya kiswahili
ABEL M MUTHEE CHUO KIKUU CHA KENYATTA

Unknown said...

Asante Abel! Karibu tukienzi kiswahili.

Anonymous said...

kazi ni mzuri cha msingi fanyeni utafiti zaidi juu ya uthibitisho kuwa kiswahili ni kibantu kwa kutumia data za kutosha

Anonymous said...

nimependa kazi yenu, inaonesha wanazuoni mnajituma.endelea kufanya utafiti juu ya hilo. JULIA N. CHARLES, CHUO KIKUU CHA DODOMA

Unknown said...

Asante, Karibu sana Bwana Charles

Unknown said...

Asante sana, Tutajitahidi kaka.

Anonymous said...

Kazi nzuri naomba utuwekee Dhana ya uunganishaji katika sentensi

Grace koki said...

kazi nzuri sana. hongera kwa ukurasa huu wenye maarifa tele. mola akuzidishie hekima na tajriba zaidi. Koki- chuo kikuu cha Kenyatta.

Unknown said...

Asante Koki!

Anonymous said...

Asanteni kwa kazi nzuri. Ningependa kufafanuliwa uhusiano wa isimu na taaluma zingine kama historia, tiba, falsafa, jamii, jiografia, saikolojia, tamaduni na dini.

Anonymous said...

SWADAKTA ASHANTENI SANA KAZII HII IHIFADHIWE KWA AJILI YA KIZAZI KIJACHO

Anonymous said...

KAZI KUNTU KABISA,HII ITASAIDIA KIZAZI KIJACHO KATIKA KUELEWA KUWA KISWAHILI NI LUGHA YA KIBANTU NA WAENDELEE KUKIGIZA NA KUKIIMARISHA.
NAMASAKA KENNEDY NAMACHI MWALIMU WA KISWAHILI KUTOKA CHUO KIKUU CHA KIMATAIFA CHA KENYATTA,KENYA.